Dr. Navanethem Pillay, Kamishina wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, hivi karibuni
alikutana na kuzungumza na Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa
Ulimwenguni na kusema kwamba, haki na amani ni chanda na pete, kamwe haviwezi kutenganishwa.
Viongozi hao wawili walishirikishana mang'amuzi na kazi zao katika mchakato wa kudumisha
haki na amani katika Jukwaa la Kimataifa, sanjari na maandalizi ya Mkutano mkuu wa
Baraza la Makanisa Ulimwenguni utakaofanyika mwezi Oktoba 2013.
Dr. Pillay
amepongeza juhudi kubwa zinazofanywa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni na kwamba,
Tamko la Haki Msingi za Binadamu lililotolewa na Umoja wa Mataifa mara tu baada ya
patashika nguo kuchanika kwenye Vita Kuu ya Pili wa Dunia, linapata chimbuko lake
katika tunu msingi za maisha ya Kikristo. Baraza la Makanisa Ulimwenguni limeendelea
kuwa ni mdau mkuu katika kuhamasisha, kulinda na kuendeleza haki na amani sehemu mbali
mbali za dunia.
Kwa upande wake, Dr. Tveit amebainisha mikakati inayoendelea
kutekelezwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika kupigania haki msingi za binadamu,
sehemu mbali mbali za dunia, kama inavyojionesha huko Pakistani na Nigeria, nchi ambazo
zimekumbwa na kinzani za kidini zinazoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu wasiokuwa
na hatia. Hii ni changamoto ya kudumisha haki msingi za binadamu na kwa namna ya pekee,
uhuru wa kuabudu ambao unafumbata haki nyingine zote!
Dr. Pillay anakiri kwamba,
Umoja wa Mataifa umeendelea kushirikiana na Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika
kuhamasisha utekelezaji wa haki msingi za binadamu hata kabla ya kuundwa kwa Tume
ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa.