2013-01-23 11:29:04

Viongozi wa kidini wanaendelea kuhamasisha ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu miongoni mwa Jumuiya ya Mataifa


Wakristo wanapoendelea kuombea umoja wa Wakristo sehemu mbali mbali za dunia, wanapaswa pia kusali kwa ajili ya kuombea: haki, amani na utu wa kila mtu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, kama njia ya kudumisha maendeleo endelevu na ustawi wa watu wote.

Kusali kwa ajili ya kuombea amani, kuwakumbusha waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai kutoka kwa Mwenyezi Mungu, chemchemi ya haki zote msingi za binadamu.

Haya ni kati ya mawazo makuu yaliyotolewa na Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, Mwakilishi wa Kudumu wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zilizoko Geneva pamoja na Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni pamoja na viongozi wa dini na madhehebu mbali mbali waliokusanyika hivi karibuni kwenye Kikanisa cha Kiekumene kwa ajili ya kuombea Umoja wa Wakristo.

Siku hii iliandaliwa na Ubalozi wa Vatican mjini Geneva, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya kuombea amani duniani, ambayo kwa kawaida inaadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe Mosi, Januari, sanjari na Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu "Theotokos". Tukio hili, limekuwa pia ni fursa nyingine lililowaunganisha kwa ajili ya kusali ili kuombea Umoja wa Kanisa, kwa kuungana na Wakristo wengine ambao tangu tarehe 18 hadi tarehe 25 Januari wanasali kwa ajili ya kuombea Umoja wa Wakristo.

Dr. Tveit anakumbusha kwamba, mbele ya Mwenyezi Mungu, binadamu wote wanajisikia kuwa ni Familia Moja ya watu wa Mungu, kama anavyokazia pia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku ya kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2013. Hii ni changamoto kwa waamini na wote wenye mapenzi mema, kusimama kidete kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, utu na heshima ya mwanadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Hii ni changamoto endelevu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Mtakatifu Yosefu, mchumba wake Bikira Maria na Baba mlishi wa Mtoto Yesu, anasema Dr. Tveit anaonesha jinsi alivyokuwa mjenzi wa amani, kwa kutunza, kulinda na kuhifadhi ya maisha ya Mtoto Yesu pamoja na Mama yake.

Ulimwengu mamboleo unawahitaji akina Mtakatifu Yosefu wengi, ili kulinda na kuendeleza maisha ya watoto hasa wale ambao bado hawajazaliwa dhidi ya utamaduni wa kifo unaowanyemelea siku hadi siku. Hawa ni watu ambao wanapaswa kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao, kwa kuendelea kuwa ni wajenzi wa haki, amani na utulivu. Ibada hii ilihudhuriwa pia na viongozi mbali mbali wa Kidini kutoka mjini Geneva na wawakilishi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa wanaoishi mjini hapo.







All the contents on this site are copyrighted ©.