Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nairobi, Jumapili, tarehe 20 Januari
2013, alimwimbia Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kutimiza miaka arobaini tangu
alipopokea Daraja Takatifu la Upadre. Ibada hii ya Misa ya Shukrani ilihudhuriwa pia
na baadhi ya wanadarasa wake waliosoma taalimungu pamoja mjini Roma, ambao wengi wao
ni Maaskofu wa Majimbo mbali mbali duniani.
Katika mahubiri yake, Kardinali
Njue alimshukuru Mungu pamoja na Familia yote ya Mungu ambayo imetembea pamoja naye
katika kipindi chote hiki cha miaka 40 ambayo kwa hakika si haba! Anamshukuru kwa
Maaskofu na Mapadre waliowekwa wakfu pamoja na ambao bado wako hai na wanaendelea
kumtumikia Mungu na jirani zao katika Daraja Takatifu la Upadre.
Kardinali
Njue anaendelea kuwataka wananchi wa Kenya kuhakikisha kwamba, wanadumisha misingi
ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa, wakati wote wa mchakato wa uchaguzi
mkuu nchini humo unaotarajiwa kufanyika hapo tarehe 4 Machi 2013. Ni wajibu wa kila
mwananchi wa Kenya kuchuchumilia haki na amani, ili kufanikisha uchaguzi mkuu ambao
mara nyingi umeacha kurasa chungu za misigano na kinzani miongoni mwa wananchi wa
Kenya.
Kardinali Njue pia anawataka wanasiasa kuendesha kampeni za kistaarabu
kwa kuheshimiana ili kutoa nafasi kwa wananchi kupima sera zitakazoweza kuwasaidia
katika mchakato wa maboresho ya maisha yao kwa siku za usoni.