Madaktari simameni kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha dhidi ya utamaduni wa
kifo kwa kuzingatia: maadili, sheria, weledi na imani!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake wa Kichungaji Dhamana
ya Afrika, "Africae Munus" anasisitizia umuhimu wa Familia ya Mungu Barani Afrika
kuhakikisha kwamba, inasimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha tangu pale
mtoto anapotungwa mimba hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu
na kamwe wasilogwe kukumbatia utamaduni wa kifo, unaofumbatwa katika sera za misaada
kwa ajili ya maendeleo Barani Afrika.
Kanisa Barani Afrika linalo jukumu muhimi
sana la kuwasaidia wanandoa wanaoshawishika kutoa mimba pamoja na kuendelea kuwa karibu
na wote waliokwisha kumbwa na mkasa huu, ili kuwasaidia kuheshimu na kuthamini zawadi
ya uhai.
Kanisa linatambua ujasiri wa serikali ambazo zimetunga sheria dhidi
ya utamaduni wa kifo wakisimama kidete kuenzi utamaduni wa uhai. Waamini wanakumbushwa
kwamba, wao wako ulimwenguni humu, lakini si wa ulimwengu, hivyo ni mwaliko wa kujichotea
nguvu na ujasiri kutoka katika Fumbo la Pasaka, yaani mateso kifo na ufufuko wa Kristo,
ili kutetea zawadi ya uhai.
Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu
Katoliki Kenya, hapo tarehe 22 Januari 2013 amezindua rasmi Chama cha Madaktari wa
Kikatoliki Kenya (Kenya Catholic Doctors Association), kwa kuwataka kusimama kidete
usiku na mchana kulinda na kutetea zawadi ya maisha, dhidi ya utamaduni wa kifo; daima
wajitahidi kuongozwa na imani, maadili ya taaluma pamoja na weledi, ili kuwatumikia
wananchi wa Kenya bila hata ya kujibakiza.
Katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani,
Madkatari wanaalikwa kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, wanatoa huduma makini,
wakisukumwa na Imani, upendo na matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa
lake.
Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Kenya kwamba, Chama cha Madaktari
Wakatoliki Kenya, kitakuwa mstari wa mbele kuwasaidia wanachama wake kutekeleza dhamana
na wajibu wao mintarafu: sheria, kanuni, maadili na imani yao, ili kuweza kukabiliana
na changamoto mbali mbali zinazoendelea kuibuliwa katika sekta ya afya na maendeleo
ya sayansi ya tiba ya mwanadamu.
Kanisa linatambua na kuthamini mchango wa
Madaktari wanaojitosa kimaso maso kuwahudumia ndugu zao hasa wale wanaoishi vijijini,
ambako watumishi wengi wa Serikali hawapendi kwenda. Kanisa nchini Kenya, limeendelea
kuwa ni mdau mkubwa wa utoaji wa huduma katika sekta ya afya, kwa kushirikiana na
Serikali.
Kwa upande wao, Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari Wakatoliki Kenya,
Dr. Stephen Kimotho Karanja amewaambia Maaskofu Katoliki Kenya kwamba, Chama chao
kimeweka kanuni msingi zinazopaswa kutekelezwa na wote wanaotaka kujiunga na Chama
cha Madaktari Wakatoliki Kenya. Kati ya masharti haya ni kutojihusisha kabisa na taasisi
au sera zinazokumbatia utamaduni wa kifo zinazojificha katika utoaji na vizuia mimba.
Hafla ya uzinduzi wa Chama cha Madaktari Wakatoliki Kenya ilihudhuriwa na
Maaskofu kadhaa pamoja na Wafanyakazi wa Sekta ya Afya nchini Kenya.