2013-01-22 09:25:31

Hotuba ya Rais Obama wakati wa kula kiapo cha Utii, Awamu ya Pili kama Rais wa Marekani


Rais Barack Hussein Obama wa Marekani, tarehe 21 Januari 2013 ameanza awamu ya pili ya uongozi wake kama Rais kwa kula kiapo cha kuilinda na kuitetea Katiba ya nchi, kama kielelezo makini cha demokrasia na Umoja wa Kitaifa, unaowafanya wote wajisikie kuwa ni raia wa Marekani. RealAudioMP3

Kila mwanadamu ana haki ya maisha, uhuru pamoja na kushiriki katika mchakato utakaompatia furaha ya kweli; mambo ambayo daima yamekumbana na kinzani, kiasi hata cha kupelekea uwagaji wa damu, ili kusimamia misingi ya haki, usawa na uhuru.

Rais Obama katika hotuba yake kwa umati wa watu uliofurika kwenye Viwanja vya Ikulu ya Marekani, amehimiza umuhimu wa kuwekeza katika sekta ya elimu, ili kuweza kukabiliana na ushindani wa haki na fursa sawa unaojitokeza katika sekta ya uchumi na soko huria; kwa kuzingatia kanuni, sheria na maadili. Wananchi wanapaswa kuwajibika pamoja na kufanya kazi kwa juhudi na maarifa, kama kielelezo cha utambulisho wao.

Katika mabadiliko yanayoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuna haja ya kujenga na kuimarisha mshikamano wa kimataifa, ili kukabiliana na changamoto zinazoibuliwa katika masuala ya kidemokrasia, elimu, uchumi na fursa za ajira. Marekani ambayo ni taifa lenye nguvu kiuchumi, lakini katika miaka ya hivi karibuni, limetikiswa na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Taifa halina budi kuwekeza katika nguvu ya vijana na kuwasaidia watu wengi zaidi kuboresha hali ya maisha yao ili kupata maendeleo ya kweli ambayo ni matunda ya kazi na malipo halali na kwamba, kila mtu anayo haki ya kuondokana na umaskini wa kipato mintarafu misingi ya uhuru na usawa mbele ya Mungu na Wanadamu. Ili kufikia malengo haya kuna haja ya kuendelea pia kuwekeza katika maendeleo ya teknolojia, ukusanyaji makini wa kodi, maboresho katika mfumo wa elimu na kuwajengea wananchi uwezo wa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa.

Rais Obama katika hotuba yake iliyokuwa inafuatiliwa na mamillioni ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, alikazia umuhimu wa kulinda usalam, kudumisha utu wa mwanadamu, usawa na uhuru kwa watu wengi zaidi na wala si kwa ajili ya kikundi cha watu wachache ndani ya Jamii, ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoweza kujitokeza. Hii ndiyo mantiki inayofumbatwa katika maboresho katika sekta ya afya na hifadhi za kijamii zinazowaimarisha kama Jamii ya wananchi wa Marekani.

Wanaharakati wa kulinda na kutunza mazingira wamempongeza Rais Obama kwa kukazia umuhimu wa kulinda na kutunza mazingira pamoja na kuwajibika barabara kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi, kwa sasa na kwa ajili ya kizazi kijacho. Athari za mabadiliko ya tabianchi zinazoambatana na: mafuriko, ukame, tufani na majanga ya moto ni changamoto ya kuwekeza katika nishati na teknolojia rafiki kwa ajili ya maendeleo endelevu, kwa kuzingatia fursa za ajira na ukuaji wa uchumi, kwa kutambua kwamba, kila mtu anahamasishwa kulinda na kutunza mazingira kama sehemu ya kazi ya uumbaji.

Rais Obama anabainisha kwamba, usalama na amani ya kudumu vina gharama yake na kwamba, umefika wakati kwa wananchi wa Marekani kuwa macho na wote wanaotaka kuwashambulia; lakini wanapaswa pia kutafuta amani na kujenga urafiki. Amerika itaendelea kuwalinda watu wake kwa njia ya silaha na utawala wa sheria; itatafuta suluhu kwa njia ya amani na kushikamana na mataifa mengine katika kudumisha misingi ya haki na amani; demokrasia na uhuru.

Nchi ya Marekani itaendelea kuwa ni chemchemi ya matumaini kwa maskini, wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili kujenga na kudumisha amani inayojikita katika misingi ya kuvumiliana, fursa sawa, utu na heshima ya mwanadamu na usawa. Hii ni safari ndefu inayopania kutoa haki na usawa kwa kuzingatia utawala wa sheria, sera makini kwa wahamiaji ili kushiriki katika maendeleo na ustawi wa Amerika pamoja na kuhakikisha usalama wa watoto wao dhidi ya mashambulizi. Kila mtu anayo haki ya kufurahia maisha.

Rais Obama anasema, amekula kiapo kwa Mungu na kwa ajili ya nchi yake, changamoto ya kuhakikisha kwamba, kweli anakuwa mwaminifu kwa Katiba wakati wote anapokuwa madarakani. Kama raia, kwa pamoja wanapaswa kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.