Kanisa Katoliki nchini Mali, limeonyesha kushakia usalama wa Wakatoliki na Wakristu
kwa ujumla, kwa kadri ghasia za mapigano zinavyoendelezwa na Wababe wa Kiislamu wenye
silaha, walioasi serikali na kutwaa baadhi ya maeneo ya nchi hiyo, hasa eneo la Kaskazini
mwa Mali.
Askofu Augustino Traore Sengue, ambaye Jimbo lake liko katika eneo
lililotekwa nyara na waasi wa Kiislamu wasiovumilia wengine, anasema , ingawa mpaka
sasa hakuna mashambulizi ya moja kwa moja katika makanisa, Wakristu wana woga mkubwa
wa kwenda kusali katika makanisa au kuadhimisha ibada zao kwa uhuru na kama wanavyopaswa.
Hivyo wengi wamefichama majumbani mwao, wakiwa wamegubikwa na woga mkubwa
wa kutoka nje. Hawana la kufanya bali kusubiri hadi hapo wenye mamlaka ya kitawala,watakapoweza
kupata suluhu ya kusitisha ukatili huo. Wakristu hao hawana uhakika na kitakacho
watokea wao wenyewe au kwa majengo ya Makanisa iwapo waasi watatwaa utawala katika
eneo la Kaskazini mwa Mali.
Askofu Augostino ameonyesha wasiwasi wa kushambuliwa
kwa makanisa na wababe hao, ingawa kwa wakati huu anasema, bado kuna mahusiano mazuri
kati ya Wakristu na waislamu wenye kuwa na kiasi. Na kwamba, wote wenye mapenzi mema
bado wanaonyesha kuwajibika na udumishaji wa umoja na mshikamano , wengi wao wakitamani
ghasia za mapigano yanayoendelea zisitishwe mara moja.
Habari inasema, kwa
wakati huu , zaidi ya raia 200,000 wa Mali wamehama maeneo yao na kuelekea maeneo
ya Kusini mwa Mali ambako kuna usalama zaidi . Na watu wengine wamevuka mpaka na kuingia
katika mataifa ya Niger, Nigeria, Burkina Faso , Morocco na Algeria.
Kanisa
Katoliki Mali , lina Majimbo sita yanayohudumia Wakatoliki wapatao asilimia mbili
ya raia wote wa Mali wapatao millioni 15.8, ambayo wengi wao ni Waislamu .
Maasi
yanayoendeshwa katika eneo la Kaskazini, yalizuka tangu March mwaka jana 2012, ambako
waasi hao wanaodai Sharia za Kiislamu zitawale, wamekwisha fanya umwagaji wa damu
mwingi na uharibifu mkubwa wa mali na kumbukumbu katika eneo hilo lenye utajiri mkubwa
wa historia.
Katikati ya mwezi huu Januari, Askofu Mkuu Jean Zerbo wa Bamako
, aliomba ujia wa usalama utolewe, kwa ajili ya upelekaji wa misaada ya kibinadamu
kwa umma unaoteswa na ghasia hizo, watu wasiokuwa na hatia hasa wanawake na watoto
.