Katiba Mpya ya Tanzania ijibu changamoto kuhusu: rushwa na ufisadi; mgawanyo wa rasilimali
za nchi; uwajibikaji na vyombo vya kusimamia na kutoa haki!
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika kuhamasisha utoaji wa maoni katika mchakato
wa kuandika Katiba mpya linabainisha kwamba, nia ya maoni haya ni kusaidia waamini
wetu kutafakari na kupata uelewa na hivyo kuweza kutoa maoni makini kwa faida ya jamii
yetu na Taifa letu. Maoni haya yamejikita hasa katika changamoto zifuatayo: Rushwa na
ufisadi
Tukumbuke Rushwa nia adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa.
Hadi sasa miaka hamsini ya uhuru wetu tunaona rushwa inazidi kukua na kuenea. Na imejikita
pia hadi kwenye vyombo vikuu vya utawala (Polisi, Mahakama, Serikali na Bunge) na
inaelekea vigumu kuidhibiti. Tatizo hili kongwe linahusu jamii nzima – kushiriki kwa
kutoa au kupokea ama kufumbia macho. Matokeo yake rushwa na ufisadi imetuathiri sote
kama wananchi na kama Taifa. Tutoe maoni yetu kuonyesha ni namna gani tatizo hili
linaweza kutatuliwa kisheria na kijamii. Tutazame upya jinsi ya kuimarisha vipengele
vya kudhibiti ukiukwaji wa maadili kwa viongozi na pia kuona kama TAKUKURU kama ni
chombo huru na chenye meno kisheria.
Mgawanyo wa mali na rasilimali
za nchi
Hizi ni pamoja na ardhi, madini, mafuta/gesi, misitu, mbuga za
wanyama, bahari, maziwa na mito, bila kusahau mfuko wa taifa (hazina). Utajiri huu
ni majaliwa ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi wa Watanzania wote kwa vizazi na
vizazi. Hali ilivyo sasa ni tofauti na azma hiyo. Wachache wamejilimbikizia na wengi
wanaendelea kuishi maisha duni, kumekuwa na mgawanyo wa matabaka ya wenye nacho na
wasio nacho. Kijumla wanyonge wametupwa pembeni katika maendeleo ya kiuchumi. Wawekezaji
kutoka nje wanapewa kipaumbele dhidi ya wananchi kwa njia ya mikataba kusainiwa katika
usiri mkubwa. Mwelekeo huu unahatarisha amani na hadi sasa kumekuwa na matukio mengi
ya uvunjifu wa amani katika jitihada za wananchi kujaribu kutetea maslahi yao. Katiba
iweke namna ya kuhakikisha wananchi wote wanashiriki katika kutumia rasilimali zetu
kwa maendeleo ya wote na kuzitunza kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Uwajibikaji
: raia na viongozi kwa ngazi na makundi yote
Kadiri siku zinavyokwenda
moyo wa uwajibikaji unaendelea kufifia tangu ngazi ya familia. Jamii inakosa kushikamana
katika kujiletea maendeleo na ustawi na hata huharibu miundombinu iliyowekwa kwa ajili
yao. Viongozi wanakiuka maadili na kuliingizia Taifa hasara kubwa na bado hakuna kuwajibika
ama kuwajibishwa. Kwa hiyo tunaona mfumo wa uwajibikaji kijumla sio mzuri. Katiba
iweke taratibu wa kung’olewa madarakani kwa sababu ya kutowajibika, iimarishe njia
za kudhibiti madaraka (checks and balance), bunge liwe kweli mwakilishi wa wananchi
na mijadala yake iongozwe katika hali ya kuruhusu maoni mbadala na kuyaheshimu. Raia
wasibaki katika kulalamika tu, bali waonyeshe mamlaka yao na nguvu yao katika suala
zima la uwajibilkaji.
Vyombo vya kusimamia na kutoa haki
Hapa
tulenge mahakama na polisi. Vyombo hivi vimeshindwa kufikia matarajio ya wananchi.
Zaidi vimekuwa upande wa wenye fedha na madaraka na kwa wananchi wa kawaida na hasa
wanyonge imekuwa ni vigumu mno kupata haki zao. Kwa upande mwingine wananchi nao wanashiriki
kuvifanya vyombo hivi vishindwe kutimiza majukumu ya uwepo wake mfano kwa njia ya
kushiriki rushwa, wakati mwingine ikiambatana na kubambikiza kesi, polisi kutesa
na kudhalilisha, kuchelewesha mno kesi na pengine hukumu ikitoka kuonyesha kuwa mhabusu
hakuwa na kosa nk. Katiba iwezeshe vyombo hivi kuwa huru na hivyo kutenda haki sawa
kwa wote badala ya kuegemea upande fulani.