2013-01-18 07:52:59

Umoja wa Wakristo ujikite katika tafakari ya kina kuhusu Mafundisho Tanzu ya Kanisa na ushuhuda katika huduma


Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican sanjari na Mwaka wa Imani anabainisha kwamba, tafsiri sahihi na makini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni tukio rejea kwa Kanisa Katoliki katika mageuzi yanayoendelea kutekelezwa na Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Kiini cha mabadiliko haya yanajionesha kwa namna ya pekee, katika Maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa.
Hapa unaweza kubainisha mageuzi ndani ya mageuzi. Tafsiri na ufahamu mpana zaidi wa Nyaraka za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni muhimu sana katika kugundua na kuenzi utajiri uliomo kwenye Nyaraka kumi na sita za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ili uweze kutumika katika kuendeleza maisha na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo.
Mageuzi ya Kiliturujia hayana budi kutazamwa katika Maadhimisho yote ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na tasiri yake makini, vinginevyo, watu wanaweza kujikuta kwamba, wanapoteza dira na lengo la Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kwa maisha na utume wa Kanisa.
Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita unalandana sana na Mwaka wa Imani uliotangazwa na Papa Paulo wa sita; kwani viongozi hawa wa Kanisa wanatumia Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kama rejea ya maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Kwa Papa Paulo wa sita, Mwaka wa Imani yalikuwa ni matokeo ya maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ameutangaza Mwaka wa Imani, kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Ni mwaliko na changamoto ya kutangaza na kutolea ushuhuda Imani kwa Kristo na Kanisa lake, kama njia ya kukabiliana na changamoto, vikwazo na fursa zinazoendelea kujitokeza katika Ulimwengu mamboleo.
Waamini wanachangamotishwa kwa njia ya ushuhuda wa imani katika matendo, kuyatakatifuza malimwengu: kwa mwanadamu kuheshimiwa na Mungu kupewa kipaumbele cha kwanza katika maisha.
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani anasema Kardinali Kurt Koch yana umuhimu wa pekee katika majadiliano ya Kiekumene na Waamini wa dini ya Kikristo. Umoja wa Wakristo unaweza kupatikana, ikiwa kama Wakristo kwa pamoja wataweza kufanya tafakari ya kina kuhusu Mafundisho Tanzu ya Kanisa na Misingi ya Imani ya Kanisa. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, katika ukame na jangwa la maisha ya watu: kimaadili na kiutu, kuna haja ya kuwa na ushuhuda wa pamoja unaotolewa na Wakristo sehemu mbali mbali za dunia.
Mageuzi ya Kiliturujia yaliyofanywa na Kanisa Katoliki ni mada inayofuatiliwa na Makanisa na Madhehebu mengine ya Kikristo, kwani wanataka kufahamu maana na umuhimu wake katika maisha na utume wa Kanisa. Mageuzi ya Kiliturujia yanayofanywa na Kanisa Katoliki yanajikita katika Fumbo la Pasaka, yaani: Mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Mageuzi haya yanafumbata kwa namna ya pekee Mapokeo ya Kanisa.
Kardinali Kurt Koch anafafanua zaidi kwa kusema kwamba, ifahamike kuwa mabadiliko ya Kiliturujia yaliyoletwa na Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, hayamaanishi kujitenga na Historia, Mapokeo na Urithi wa utajiri wa Kanisa kwa miaka iliyopita. Bali haya ni maboresho ya maisha na utume wa Kanisa, katika kusoma alama za nyakati, maneno yaliyopewa msukumo wa pekee na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu; kulinda na kutetea ut una heshima ya mwanadamu; kutafuta mafao ya wengi; haki, amani na mshikamano; Mwenyezi Mungu akipewa kipaumbele cha kwanza katika maisha na mikakati ya binadamu katika ulimwengu mamboleo.







All the contents on this site are copyrighted ©.