Tafakari ya Neno la Mungu Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa: Mkaribisheni
Yesu katika Familia zenu kwani ni chemchemi ya furaha ya kweli!
Mpendwa mwana wa Mungu, Dominika iliyopita tulisherehekea Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana,
sikukuu ambayo ilihitimisha kipindi cha Noel na shamrashamra za Mwaka Mpya. Ni sikukuu
ambayo pia huchukua nafasi ya Dominika ya kwanza ya kipindi cha kawaida cha Mwaka
wa Kanisa, kumbe leo tunatafakari masomo ya Dominika ya II ya kipindi cha mwaka Che
wa Kanisa. ambayo yatuongoza kutambua kuwa Bwana yu katikati yetu na ndiyo furaha
yetu.
Nabii Isaya
katika somo la kwanza anatangaza upendo wa Mungu kwa taifa la Israel. Kama tunavyofahamu,
Mungu alimwahidi mfalme Daudi kuwa katika ukoo wake utatokea mwangaza utakaokuwa kwa
ajili ya wokovu wa ulimwengu. Kwa zawadi hii kwa mfalme Daudi watu wote watauona utukufu
wa Mungu. Nabii Isaya anatoa mfano wa Bwana na Bibi arusi wanavyopendana ndivyo ambavyo
Mungu analipenda taifa la Israeli na watu wake wote. Kwa zawadi hii, mzaburi wa Zaburi
ya 95 anatualika kumwimbia Bwana wimbo mpya na kuhubiri habari za utukufu wa Mungu
kwa mataifa yote
Mtume Paulo anapowaandikia Wakorinto katika somo la pili anataka
kusisitiza nguvu ya Mungu Roho Mtakatifu anayegawa vipaji vyake kadiri apendavyo kwa
kila mmoja wetu. Kwa kugawa vipaji kwa kila mmoja anataka kutuonjesha uzuri wa maisha
ya jumuiya, maisha ya kusaidiana. Ndiyo kusema vipaji si zawadi binafsi bali ni kwa
ajili ya kuwafaidia wengine. Mtume Paulo anasema, pana tofauti ya karama lakini mgawaji
wa mapaji hayo ni mmoja yaani Roho Mtakatifu.
Mama Kanisa katika hili daima
yuko makini kuongoza taifa la Mungu ili lisije likaanguka katika kiburi cha majivuno!
Katika historia na hata zama zetu wapo baadhi yetu ambao hujisikia kama vile wao ndio
Roho Mtakatifu! Kwa kutafakari somo hili tunaalikwa kuwa makini katika kutumia zawadi
tulizopewa na hasa kwa ajili ya kufaidia taifa la Mungu na si kwa faida binafsi.
Mpendwa
mwana wa Mungu sehemu ya Injili tunayoitafakari leo yaani Injili ya Yohane 2:1-12
tunasikia habari ya arusi ya Kana ya Galilaya. Kristo aliyejitangaza waziwazi katika
sherehe ya Tokeo la Bwana anazidi kujionesha wazi katika umungu wake na unyenyekevu
wake, na zaidi katika uchungaji wa taifa lake.
Mpendwa mwanatafakari, hebu
tujiulize, kama ingetokea mtu mmoja akamwuliza Myahudi, wapi Mungu anaishi au wapi
tunaweza kukutana na Mungu, unatarajia Myahudi huyu angejibu nini? Kwa vyovyote vile
Myahudi angesema Mungu anakaa katika Hekalu la Yerusalemu au anakaa mlimani! Leo baada
ya kusikia sehemu ya Injili ya Yohane juu ya arusi ya Kana ukiulizwa utatoa jibu lilelile
la Myahudi?
Natumaini jibu letu linapaswa kuwa kama inavyojionesha katika
Injili, yaani Mungu tunaweza kumpata mezani petu tunapokula chakula, katika sherehe
yetu ya ndoa na katika Misa Takatifu. Kumbe, tunaweza kusema kuwa arusi ya Kana ni
kielelezo cha uwepo wa Bwana katikati ya maisha yetu, ambaye ndiye yule Emanueli,
yaani Mungu pamoja nasi. Bwana yu katikati ya watu wanaofurahi na kuchangamka katika
maisha yao.
Katika arusi ya Kana Bwana anafungua namna mpya ya kuwa katikati
ya waamini, anafurahi na waamini na si tu katika furaha ya kiroho bali pia katika
furaha inayogusa maisha ya kawaida. Jambo la namna hii latukumbusha fikira za Mtakatifu
Katarina wa Siena aliyekuwa akimwomba Mungu atuondolee maisha yanayojionesha katika
sura zilizojaa huzuni! Kwa tendo la Bwana pale Kana hali ya maisha ya watu imeinuliwa
juu ili yawe kweli maisha ya furaha.
Katika arusi ya Kana tunaona jambo jingine
la kutufanya tufikiri na kutafakari juu ya maisha yetu na uwezo wa Mungu kati yetu.
Jambo lenyewe ni kuishiwa Divai. Wote twafahamu kuwa Divai ni alama ya furaha na shamrashamra
katika maisha ya Kiyahudi. Kwisha kwa Divai maana yake kwisha kwa furaha! Bwana yupo
pale pamoja na wanaarusi, anaona Divai imeisha!
Hapa twajifunza kuwa Yesu
hayuko pale kushiriki furaha tu bali hata kupokea na kushiriki machungu ya maisha
ya watu. Hata hivyo atabadirisha machungu haya na kuyafanya yawe furaha! Anageuza
maji na kuwa divai. Mpendwa mwujiza wa kwanza! Divai ni nzuri kupindukia na furaha
inatokea si kinyume cha furaha ya mwanzo bali anakamilisha furaha hiyo. Mpendwa Bwana
aweza kubadili maisha yako ya uchungu kuwa furaha, cha msingi mwambie Maria, sina
divai!
Mama Maria anawaambia watumishi fanyeni yale atakayosema na wanafanya
hivyo! Sisi leo tunaalikwa kufanya anayosema Bwana katika Neno lake na hapo ndipo
kuna furaha sasa na hata milele. Katika kupata furaha hii tunahitaji kushiriki kikamilifu
kazi nzima hata kama ni ngumu! Divai ya furaha ni tunda la kushirikishana pamoja vipaji
kati ya watu mbalimbali.
Tunamwona Mama wa Mungu, watumishi wa sherehe, mwenye
kuongoza arusi kila mmoja anafanya sehemu yake kadiri ya kipaji alichopewa na Mungu
kadiri tulivyosikia katika somo la II, Mtume Paulo akifundisha juu ya karama zitokazo
kwa Roho Mtakatifu kwa ajili ya kufaidiana. Mpendwa yafaa tukumbuke kwamba kitovu
cha furaha yote baada ya kushirikishana yote ni Bwana wetu Yesu Kristo. Yeye kadiri
ya Nabii Isaya ndiye ambaye hawezi kumwacha awaye yote katika taabu bali atamfanya
angae mbele ya mataifa.
Ninakutakieni furaha tele katika maisha yako ukikumbuka
kuwa Bwana ndiye mchungaji mwema, ndiye chanzo na mwisho wa furaha na amani ktk maisha
yetu na daima ukimwalika pamoja na Mama Maria atakuwa nawe kukuinua na kukusaidia
ukakue katika furaha na kisha uzima wa milele. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari
hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya, C.PP.S.