Matumaini ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio De Janeiro
Katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio de Janeiro kuanzia
tarehe 23 hadi 28 Julai 2013, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anatarajiwa
pia kupata fursa ya kujionea mwenyewe mandhari ya mji wa Rio de Janeiro, wakati atakapokuwa
anazungushwa na Helikopta.
Hayo yamesemwa na Askofu mkuu Oran Joao Tempesta
wa Jimbo kuu la Rio de Janeiro ambaye yuko hapa mjini Vatican hadi hapo tarehe 25
Januari, 2013 kushiriki katika vikao mbali mbali na Mabaraza ya Kipapa kama sehemu
ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013, ambayo Kanisa
Katoliki Brazil ni mwenyeji wake.
Inakadiriwa kwamba, vijana zaidi ya millioni
mbili kutoka sehemu mbali mbali za dunia watashiriki katika kilele cha maadhimisho
haya. Vijana watakuwa na fursa ya kufanya Njia ya Msalaba ambayo imekuwa na mvuto
mkubwa katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Kimataifa, kama kielelezo cha ushuhuda
wa Imani yao kwa Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka wafu, ili kuwakirimia
waja wake maisha ya uzima wa milele. Njia ya Msalaba itafanyika kwenye Fukwe maarufu
za Copacabana, Brazil.
Kamati ya Maandalizi kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki
Brazil inaendelea kushirikiana na Mabaraza na vitengo mbali mbali vinavyohusiana na
hija za kichungaji za Khalifa wa Mtakatifu Petro, ili kukamilisha mambo yote kwa wakati
muafaka. Maandalizi haya yanawashirikisha pia viongozi mahalia kutoka Brazil kwani
hata wao watakuwa nafasi ya pekee katika hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, nchini Brazil.
Itakumbukwa kwamba, Maadhimisho ya Siku ya
Vijana Duniani yanasimamiwa na kuendeshwa na Baraza la Kipapa la Walei. Katika Liturujia
ambamo Baba Mtakatifu anatarajiwa kushiriki, Mshereheshaji Mkuu wa Kipapa anahusika
moja kwa moja, bila kusahau mawasiliano, ulinzi na usalama.
Baba Mtakatifu
anatembelea Brazil si tu kama mkuu wa Nchi ya Vatican, bali pia kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro anayekwenda kuwaimarisha ndugu zake katika Imani na kuwapatia vijana matumaini
mapya ya kuendelea kuwa ni wadau wakuu katika azma ya Uinjilishaji Mpya, changamoto
inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa wakati huu.