Wanasiasa msitatute umaarufu kwa rasilimali ya Tanzania kwani ni mali ya watanzania
wote!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amekemea tabia ya baadhi
ya viongozi wa kisiasa kutumia suala la raslimali za taifa, ikiwamo gesi asilia kujifatufia
umaarufu wa kisiasa na kuwapotosha wananchi. Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa ni jambo
la hatari na lisilo na tija kwa wanasiasa kujaribu kuigawa nchi vipande vipande kwa
sababu ya kujitafutia umaarufu kwa kutumia raslimali za taifa.
Rais Kikwete
ameyasema hayo, Januari 15, 2013 wakati alipokutana na Balozi wa Uingereza nchini
ambaye anamaliza muda wake, Mheshimiwa Dianne Corner ambaye alifika Ikulu, Dar Es
Salaam kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa uwakilishi katika Tanzania. Rais Kikwete
na Balozi Corner wamezungumzia masuala mbali yanayohusu uhusiano kati ya Tanzania
na Uingereza, masuala ya ukanda wa Afrika Mashariki na masuala ya kimataifa.
Kuhusu
ugunduzi wa gesi asilia uliofanywa na Kampuni BG ya Uingereza katika eneo la Msimbati
kwenye Bahari ya Hindi, walikubaliana kuwa hilo ni jambo jema na lenye kuleta matumaini
kwa Tanzania hasa wakati itakapoanza kuvunwa katika miaka michache ijayo. Kuhusu siasa
zilizoanza kujitokeza kufuatia ugunduzi huo mkubwa wa gesi asilia, Rais Kikwete amesema
kuwa ni tabia ya hatari kwa wanasiasa kutumia gesi asilia hiyo ama raslimali nyingine
kujijengea umaarufu wao ambao umeporomoka.
“Unawezaje kuwa na nchi moja na
taifa moja wakati kila mmoja anadai raslimali kutoka kwenye eneo moja ibakie na kunufaisha
watu wa eneo hilo tu. Huwezi kuwa na nchi moja na yenye umoja wakati kuna nchi ya
gesi asilia kule Mtwara, kuna nchi ya kahawa kule Kilimanjaro, kuna nchi ya chai na
ndizi kule Bukoba,” amesema Rais Kikwete na kuongeza: “Kwa sababu kama gesi asilia
inatakiwa kubakia na kunufaisha watu wa Mtwara tu, basi wenye haki zaidi ya kudai
jambo hili siyo watu wa Mtwara bali ni watu wa Msimbati ambako ndiko ilipogunduliwa
kesi ambako ni maili 60 kutoka Mtwara, kilomita 200 kutoka Newala.”
Ameongeza:
“Unajua nchi yetu inao baadhi ya wanasiasa wenye uchu wa umaarufu na ambao wanatumia
jambo hili jema kwa manufaa yao binafsi bila kujali umoja na jadi ya taifa letu la
raslimali zetu kutumika kuiendeleza nchi nzima.” Kuhusu uhusiano kati ya Tanzania
na Uingereza, Rais Kikwete amemshukuru Balozi Corner kwa kazi nzuri ya kuimarisha
uhusiano huo. “Umeufikisha uhusiano wetu kwenye hatua ya juu kabisa na tunakushukuru
kwa jambo hili.” Mheshimiwa Corner ambaye amekuwa Balozi wa Uingereza nchini Tanzania
kwa miaka minne amehamishiwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).