Sheria ya nchi isikumbatie utamaduni wa kifo kwa kisingizio cha kuokoa maisha ya Mamamjamzito!
Baraza la Maaskofu Katoliki Ireland linabainisha kwamba, maisha ya Mama na Mtoto ambaye
yuko bado tumboni ni matakatifu na yanapaswa kutunzwa na kuheshimiwa kikatiba na kamwe,
sheria za nchi zisikumbatie utamaduni wa kifo, kwa kisingizio cha kuokoa maisha ya
Mama mjamzito peke yake. Katiba ya Ireland inakataza utoaji mimba kwa hiyari, lakini
inaruhusu mimba hiyo itolewe ikiwa kama maisha ya Mamamjamzito yako hatarini.
Kuna
matukio kadhaa ambayo yameendelea kutokea nchini Ireland kiasi cha kuwafanya Maaskofu
Katoliki kuibua tena mjadala wa sheria ambayo itaheshimu zawadi ya maisha ya Mama
na Mtoto ambaye bado yuko tumboni, kwani hii ni sehemu ya haki msingi wa binadamu.
Askofu Christopher Jones, Mwenyekiti wa Tume ya Ndoa na Familia, Baraza la Maaskofu
Katoliki Ireland anasema kwamba, utoaji wa mimba ni mauaji ambayo kamwe hayawezi kuhalalishwa
kisheria na ni kinyume cha maadili na utu wema.
Kutokana na kushamiri kwa utamaduni
wa kifo, baadhi ya wahudumu wa sekta ya afya wamejikuta wakishinikizwa kutoa mimba
kwa kisingizio cha kutaka kuokoa maisha ya Mamamjamzito. Madaktari wanapaswa kutambua
kwamba, wao ni wadau wakuu wa maisha, hivyo ni jukumu lao kuhakikisha kwamba, wanajitahidi
kuokoa maisha ya mama na mtoto ambaye bado yuko tumboni mwa mama yake, kwani maisha
ya watu hawa ni matakatifu, yanapaswa kuheshimiwa na kulindwa kikatiba.
Majadiliano
yote haya hayana budi kutoa kipaumbele cha pekee kwa wanawake, kwa kuwaelewa, kuwahurumia
na kuwaheshimu katika shida na mahangaiko yao ya ndani. Hakuna sababu za msingi zinazoweza
kupelekea watu kutaka kukumbatia utamaduni wa kifo. Wananchi wa Ireland wanataka sasa
Serikali iitishe kura ya maoni ili kutengua sheria inayoruhusu utoaji mimba kwa kisingizio
cha kutaka kuokoa maisha ya mamamjamzito. Inasikitisha kuona kwamba, kuna zaidi ya
wanawake elfu nne kutoka Ireland wanaojihusisha na suala la utoaji mimba nje ya nchi
yao.