2013-01-15 08:13:48

Maelfu ya watu wajimwaga barabarani kutetea msingi bora wa ndoa na familia!


Takribani watu millioni moja kutoka sehemu mbali mbali za Ufaransa, Jumapili, tarehe 13 Januari 2013 walifanya maandamano makubwa kupinga muswada wa sheria unaotaka kuruhusu watu wa jinsia moja kuoana kama Bwana na Bibi na hivyo pia kuruhusia kuasi watoto. Umati huu wa watu ulikusanyika kama kielelezo cha Jamii inayothamini na kuenzi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, inayojengeka katika uhusiano wa dhati na unaowajibisha kati ya Bwana na Bibi.

Watu wanasema wanaunga mkono ndoa asilia inayoundwa kati ya Bwana na Bibi, ndiyo maana wamejitokeza kwa wingi kupinga vitendo vinavyokiuka utu na heshima ya binadamu kwa kisingizio cha uhuru na haki sawa. Haya ni maandamano yaliyowashirikisha watu kutoka dini na madhehebu mbali mbali, wote wakiwa na lengo la kusimama kidete kutetea misingi bora ya ndoa na familia, dhidi ya mmong'onyoko wa maadili na utu wema, unaoendelea kujitokeza kwa mwamvuli wa uhuru na haki msingi za binadamu.

Wananchi wa Ufaransa wanabainisha kwamba, Serikali inapaswa kuwa makini katika masuala yanayogusa: Ndoa na Familia; Haki Msingi za Watoto pamoja na kujenga utamaduni wa upatanisho wa kitaifa, ili wananchi waweze kuendelea kuishi kwa amani na utulivu.







All the contents on this site are copyrighted ©.