Huduma ya upendo ni kiini cha maisha na utume wa Kanisa
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita ameelezea nia yake binafsi inayoonesha kwamba
huduma ya upendo ni kiini cha maisha na utume wa Kanisa. Mama Kanisa anatekeleza wajibu
na utume wake kwa kuzingatia misingi mikuu mitatu: Kutangaza Neno la Mungu; kuadhimisha
Sakramenti za Kanisa na huduma. Mambo haya matatu yanakwenda pamoja na kamwe hayawezi
kutenganishwa.
Huduma ya
upendo ni alama makini ya utume wa Kanisa na utambulisho wake. Kumbe, waamini wote
wanawajibu wa kutekeleza katika maisha yao amri ya upendo ambayo Yesu mwenyewe amewaachia
wafuasi wake; kwa kuwasaidia watu katika mahitaji yao ya kimwili na kiroho.
Kanisa
katika ujumla wake anasema Baba Mtakatifu, linatakiwa kutekeleza huduma ya upendo
kuanzia katika Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo, kwenye Makanisa mahalia hadi kufikia
ngazi ya Kanisa la Kiulimwengu. Hali hii inahitaji kwa namna ya pekee uratibu wa shughuli
hizi kwa ajili ya Jumuiya, kwa kuwa na taasisi ambayo itaratibu mikakati yote.
Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anabainisha kwamba, katika Waraka wake wa kichungaji,
Mungu ni Upendo, alielezea kuwa, kadiri ya mpango wa Kanisa unaosimikwa kwa Maaskofu
ambao ni waandamizi wa Mitume, wanao wajibu wa kutekeleza huduma ya upendo katika
Majimbo yao mintarafu Sheria za Kanisa, ambamo kunapembuliwa kwa mapana utume wa Askofu
mahalia.
Maaskofu wanao wajibu mkubwa kwa Kanisa zima kuhakikisha kuwa, wanatekeleza
asili ya Kanisa katika utoaji wa huduma ya upendo kadiri ya dhamana na wajibu wa Askofu
mahalia, kwa kuzingatia sheria hasa pale anapotekeleza wajibu huu kwa kuungana na
Maaskofu wengine.
Baba Mtakatifu kwa waraka huu anapenda kutangaza rasmi nia
yake inayotoa mwelekeo wa kisheria utakaoratibu shughuli zote za huduma ya upendo
zinazotolewa na kikanisa ambazo ziko karibu na asili ya Kanisa katika kuhudumia pamoja
na utume wa Kiaskofu. Huduma ya upendo haitaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa ikiwa
kama hailengi kuonesha upendo kwa binadamu, upendo unaorutubishwa kwa kukutana na
Kristo.
Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki yanayojihusisha na matendo
ya huruma, yasijikite tu katika kutafuta na kugawa fedha kwa ajili ya huduma, bali
yaguswe na mahitaji ya watu kwa kuwamasisha waamini kutambua umuhimu wa kushirikishana,
kuheshimiana na kupendana mintarafu moyo wa Injili ya Kristo.
Mashirika ya
Misaada ya Kanisa Katoliki yajitofautishe na mashirika mengine ya misaada ya kijamii
kwa kuwa makini na huduma wanaozotoa kwa wahitaji na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii. Huduma hizi zinaweza kuwa ni katika ngazi ya Kiparokia, Kijimbo, Kitaifa
na Kimataifa. Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas ni mali ya Kanisa na
limepata mafanikio makubwa, linaheshimiwa na kuthaminiwa na waamini pamoja na watu
wengine sehemu mbali mbali za dunia kutokana na ukarimu kama kielelezo makini cha
imani kwa kujibu kwa wakati muafaka mahitaji ya maskini.
Kutokana na mwelekeo
kama huu, waamini wengi wameanzisha Mashirika ya misaada ambayo ni kielelezo cha huduma
ya upendo kwa wahitaji. Mashirika haya yanatofautiana katika asili na sharia, ingawa
yanaoneshwa jinsi ambavyo yanahitaji kujibu kilio cha huduma ya upendo kwa wahitaji.
Baba
Mtakatifu anasema Mashirika haya hayana budi kuratibiwa na Kanisa kama kielelezo cha
viongozi wa Kanisa kutambua na kuthamini mchango wa waamini walei katika maisha na
utume wa Kanisa; kwa kuheshimu sheria na kanuni husika, uongozi uliopo kama kielelezo
cha uhuru wa Wabatizwa. Itakumbukwa kwamba, Kanisa Katoliki lina taasisi zake linaloratibu
misaada inayokusanywa kutoka kwa waamini mbali mbali; taasisi hizi zinafuata sheria
na uongozi unaoziwezesha kujibu kwa uhakika mahitaji ya watu.
Baba Mtakatifu
anasema, Mashirika yote haya katika utekelezaji wa majukumu yake, hayana budi kufuata
Mafundisho ya Kanisa, Nia ya wahisani pamoja na kuzingatia sheria za nchi pamoja na
Sheria za Kanisa kutokana na wajibu ambao wahusika wanajitwalia, licha ya kuonesha
tofauti mbali mbali. Sheria zinahitajika kama sehemu ya utekelezaji wa haki na dhamana
ya Maaskofu mahalia kwa waamini wao kwa kuheshimu uhuru wa kila taasisi.