Umuhimu wa kuwekeza katika elimu kama njia ya kudumisha misingi ya haki, amani na
maendeleo endelevu
Uwekezaji katika sekta ya elimu Barani Afrika, Asia na kwa nchi zilizoko Amerika ya
Kusini ni sehemu ya mchakato unaopania kuwajengea wananchi hao uwezo wa kupambana
na umaskini na maradhi pamoja na kuunda mfumo wa sheria ulio sawa na unaozingatia
utu na heshima ya binadamu. Lengo ni kuhakikisha
kwamba haki inatendeka, kwa kuwa na mifumo makini ya uchumi. Haki inaweza kutendeka
pale tu watu wenyewe wanatambua na kuheshimu haki msingi. Hivyo basi, ujenzi wa msingi
wa haki na amani hauna budi kujielekeza katika kuwaandaa watu kupambana kufa na kupona
dhidi ya rushwa, ufisadi na matendo ya jinai; biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja
na kuondokana na mambo yote ambayo yanaendelea kujenga hofu na migawanyiko mbali mbali
ndani ya Jamii, kwani yote haya ni kikwazo cha maendeleo endelevu, amani na utulivu
katika Jamii. Ni changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita kwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa mjini Vatican, wakati wa
salam na matashi mema kwa Mwaka 2013. Anasema, amani inawekwa katika mtihani mkubwa
kutokana na mambo ambayo yanaendelea kutishia uhuru wa kidini, jambo ambalo Jumuiya
ya Kimataifa haijalipatia umuhimu wa kutosha. Matokeo yake, baadhi ya watu wanakosa
uvumilivu na kuanza kushambulia watu, alama za kidini na utambulisho wa Mashirika
ya kidini. Baadhi ya waamini na kwa namna ya pekee, Wakristo hawashirikishwi katika
kuchangia mafao ya wengi kwa njia ya taasisi zao za elimu na huduma za kijamii. Ili
kulinda na kudumisha uhuru wa kidini anasema Baba Mtakatifu, kuna haja ya kuheshimu
dhamiri za watu, kwani unagusa masuala muhimu sana ya kimaadili na kidini yanayofumbatwa
katika utu na heshima ya binadamu. Hizi ni nguzo msingi na utambulisho wa taasisi
na uhuru wa kidini. Nguzo hizi zisipoheshimiwa na kuthaminiwa, matokeo yake ni watu
kushindwa kuvumiliana na amani inaweza kutoweka. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita, anabainisha kwamba, ujenzi wa amani hauna budi kujikita katika majadiliano
pamoja na kujikita katika maboresho ya mahusiano kati ya Serikali na Kanisa. Tamko
la Baraza la Maaskofu Katoliki Poland, Patriaki wa Moscow pamoja na Serikali ya Russia
na Poland ni mfano wa kuigwa. Kuna mifano mingi ya kuigwa katika majadiliano ya kidini
kutoka Mindanao, Ufilippini. Amani inakamilishwa kwa njia ya upendo na haki; mambo
ambayo ni msingi wa utume wa kidiplomasia unaotekelezwa na Vatican, sehemu mbali mbali
za dunia. Hiki ni kipaumbele cha kwanza cha Kanisa Katoliki, kwani haki na amani ni
chanda na pete. Mama Kanisa anatekeleza wajibu huu kwa njia huduma zinazojionesha
kwa namna ya pekee katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu ya Jamii. Kanisa
limeendelea kuwasaidia wakimbizi wanaolazimika kuyahama makazi yao kutokana na vita
na sasa Kanisa linajielekeza katika kuwahudumia watu waliokumbwa na maafa asilia,
sehemu mbali mbali za dunia. Matukio yote haya yajenge na kuimarisha moyo wa upendo
na mshikamano unaoongozwa na kanuni auni. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita
anasema kuwa, imekwisha gota miaka hamsini, tangu Papa Paulo wa Sita, alipowahimiza
Viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kuwa kweli ni wajenzi wa haki na amani, changamoto
endelevu hata kwa Mabalozi na wawakilishi wa nchi na Mashirika ya Kimataifa sehemu
mbali mbali za dunia.