Kampeni ya kuombea Miito Mitakatifu nchini Marekani yaanza rasmi
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani limeanza kampeni ya Juma zima, ili kuhamasisha
miito mitakatifu ndani ya Kanisa, kuanzia tarehe 13 Januari 2013 hadi tarehe 20 Januari
2013. Kampeni hii inalenga zaidi miito ya: Kipadre, Kitawa na Maisha ya Kuwekwa Wakfu.
Hiki ni kipindi ambacho waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee, kusali kwa ajili
ya kuombea miito kwa kutambua kwamba, mavuno ni mengi lakini watenda kazi katika shamba
la Bwana ni wachache. Waamini wanapaswa kuelimishwa ili kusaidia mchakato wa Kanisa
kuwapata viongozi waaminifu, wachamungu na watakatifu watakaojitoa kwa ajili ya kumtumikia
Mungu na jirani zao katika maisha na utume wa Kipadre na kitawa. Askofu mkuu Robert
Carlson anasema kwamba, hili ni tukio muhimu sana wakati huu Mama Kanisa anapoendelea
kuwahamasisha waamini kuonesha ushuhuda wa imani thabiti, ari na moyo mkuu katika
maisha na utume wa kimissionari, kama sehemu ya utekelezaji wa changamoto zilizotolewa
na Mababa wa Sinodi ya Uinjilishaji Mpya, iliyohitimishwa mjini Vatican, hapo Mwaka
2012 na kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Mama Kanisa bado anayo dhamana
ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa ujasiri mkuu na kuwashirikisha wengine ile
furaha ya kukutana na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia; lakini kwa namna ya ajabu kabisa,
furaha hii inajionesha katika kuwahudumia wengine katika huduma za kipadre na kitawa.
Dunia ina kiu na njaa ya kusikiliza Habari Njema ya Wokovu, kumbe, kuna haja ya kuwa
na Mapadre na Watawa watakaojitoa kimaso maso kutangaza Injili ya Kristo kwa ujasiri
mkuu wakati huu wa mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo. Tafiti zilizofanywa
hivi karibuni nchini Marekani zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya vijana wapatao 600,
000 wenye umri kati ya miaka 14 hadi 35 wanaonesha hamu ya kutaka kuwa Mapadre na
Watawa. Maaskofu Katoliki Marekani, wanasema, hii ni habari njema na kwamba, Waamini
wanayo dhamana ya kusali kwwa ajili ya kuombea miito mitakatifu ndani ya Kanisa sanjari
na wao wenyewe kujitoa kimasomaso kwa ajili ya utume huu. Kanisa halina budi kuendelea
kuwahamasisha vijana kufahamu umuhimu wa maisha na utume wa Kipadre na Kitawa ndani
ya Kanisa. Kwa mara ya kwanza, Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, lilianzisha
Siku ya Kuombea Miito Mitakatifu kunako mwaka 1976, kwa kutenga Jumapili ya 28 ya
Kipindi cha Mwaka kuwa ni Siku Maalum ya Kuombea Miito Mitakatifu. Kunako mwaka 1997,
Siku hii ikabadilishwa, ili kwenda sanjari na Sherehe za Ubatizo wa Bwana. Kwa mwaka
2013, Sherehe hii inaangukia tarehe 13 Januari 2013. Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani,
limeamua kwamba, kuanzia Mwaka 2014, Juma la kuombea Miito Mitakatifu ndani ya Kanisa,
litafanyika Juma la kwanza katika Mwezi Novemba, kila mwaka.