Mfalme Alberto II akutana na Baba Mtakatifu Benedikto XVI mjini Vatican
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumamosi, tarehe 12 Januari 2013 amekutana
na kuzungumza na Mfalme Alberto wa Pili kutoka Monaco pamoja na ujumbe wake; ambao
pia ulipata nafasi ya kukutana na kufanya mazungumzo na Kardinali Tarcisio Bertone,
Katibu mkuu wa Vatican pamoja na Askofu mkuu Dominic Mamberti, Katibu mkuu wa mambo
ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.
Katika mazungumzo
ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita na Mfalme Alberto wa Pili, wamejadili
kwa kina na mapana kuhusu mchango wa Kanisa Katoliki katika ustawi na maendeleo ya
wananchi wa Monaco. Viongozi hawa pia wamegusia kuhusu masuala mbali mbali ya kimataifa:
maendeleo endelevu ya watu; matumizi sahihi ya rasilimali pamoja na utunzaji bora
wa mazingira.