Watambue maadui wakuu wa Katiba ya Nchi ambayo ni Sheria Mama: wanasiasa na Wananchi
wenyewe!
Wakati tukiwa katika harakati za kushiriki haki yetu ya kikatiba ya kutoa maoni katika
utunzi na uandishi wa Katiba Mpya ya Tanzania, Padre Liston Lukoo anapenda kuwashirikisha
watanzania alichosema Bwana Roberto Benigni, msanii marufu sana nchini Italia. Siku
chache kabla ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012, Bwana Robert Benigni
alikuwa na kipindi katika moja ya Luninga za Italia kuhusu Katiba ya Italia.
Kati
ya mambo muhimu sana alivyoongelea katika lugha ya sanaa ni Katiba ya Italia na vipengele
vyake kumi na viwili. Alitaja wazi kuwa Katiba ya nchi ni rafiki ya raia, inapaswa
kuwalinda na kuwatetea. Hivyo, Katiba yoyote inapaswa kuwa ni kwa maslahi na mali
ya wananchi wote.
Bwana Benigni katika onesho hilo ambalo lilikuwa na mvuto
mkubwa kutokana na umuhimu wa mada aliyokuwa anazungumzia aliwataja maadui wawili
wa Katiba yoyote ile kuwa ni WANASIASA NA WANANCHI WENYEWE.
MOJA: WANASIASA
ni maadui wa kwanza wa Katiba kwani mara nyingi hujitahidi kutunga Katiba kwa faida
yao wenyewe na kusahau wananchi wanaopaswa kuwahudumia. Kwa namna hiyo, wakiachiwa
wanasiasa watunge Katiba, si rahisi kupata Katiba yenye kutenda haki na kutetea masilahi
ya wengi. Ndiyo maana katika nchi ambazo wanasiasa wamekuwa ni waandishi wa Katiba,
katiba haiwezi hata siku moja kujitosheleza.
MBILI: WANANCHI: Hawa na hasa
wale ambao hawashiriki chochote katika kuandaa Katiba, kuisimamia na kuitekeleza ni
maadui wakubwa pia wa Katiba yoyote ile. Hivyo mwananchi ambaye hafanyi lolote linalohusu
ustawi wa nchi yake kupitia Katiba halali, anakuwa ni adui mkubwa wa Katiba husika,
kwani, kwa kufanya hivyo anawaachia wanasiasa kufanya yale yanayowapendeza wao na
kwa ajili ya masilahi yao.
Yatokanayo: Kwa mantiki hiyo, wakati huu ambao Tanzania
inajiandaa kuandika na kutunga Katiba mpya upo uwezekano mkubwa, na lazima tuseme
kuwa wapo maadui hao wawili. Wapo wanasiasa ambao wangependa Katiba ijayo iwe kwa
maslahi yao. Hao ni adui wa nchi na wananchi kwa ujumla.
Lakini adui mkubwa
kabisa ni wananchi wenyewe ambao hudhani kuwa mchakato huu wa Katiba hauwahusu. Ni
ule msemo husemao "Mimi simo". Na bahati mbaya sana hao wasemao "Mimi simo" ni wale
wenye uelewa mkubwa na nafasi muhimu katika jamii. Je, mambo yakienda ndivyo, sivyo
nani wa kulaumiwa: Maadui wanasiasa au maadui wananchi?
Bwana Roberto Benigni
alisema kuwa kutowajibika kikatiba ni uadui mkubwa wa Katiba husika. Watanzania tumepewa
nafasi hii kuitumia, lakini huenda hatujui umuhimu wa nafasi hii katika ustawi wa
jamii yetu. Ili kuepuka kuwa maadui wa Katiba, inafaa katika muda huu kila mmoja achukue
nafasi yake, na zaidi sana kujiandaa kwa makini sana katika kupigia kura ya NDIYO/SIYO
Muswada wa Katiba mpya kadiri utakavyoletwa kwa wananchi.
Tukumbuke kuwa kutopiga
kura ni UADUI MKUBWA WA KATIBA ULIOPITILIZA maana ni kwa njia ya kupiga kura ndiyo
tunapata nafasi ya kumshinda adui namba moja: WANASIASA ambao wangependa Katiba iwanufaishe
wao na kikundi kidogo cha watu ndani ya Jamii.
Tutoe maoni ya KATIBA MPYA:
kwa kuzingatia: maisha ya mtu, mafao ya wengi, utu na heshima ya mwanadamu, uhuru
wa kuabudu; umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa; udini, ukabila, umajimbo havina
nafasi katika ujenzi wa Sheria Mama ambayo ni Katiba ya Nchi.