2013-01-11 11:35:47

Mshikamano wa kimataifa katika maboresho ya huduma ya elimu, afya ba maji safi na salama nchini Haiti!


Shirika la kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF, katika utafiti wake, lina bainisha kwamba, katika kipindi cha miaka mitatu tangu tetemeko la ardhi lilipotokea nchini Haiti, kumekuwepo na maendeleo makubwa katika huduma kwa watoto hasa katika sekta ya elimu, afya na lishe.

Idadi ya watoto wenye umri wa miaka sita hadi kumi na mmoja, wanaosoma shule za msingi wanaendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka na kwamba, vifo vya watoto wachanga chini ya miaka mitano vimepungua kwa asilimia ishirini, kati ya Mwaka 2005 hadi mwaka 2012. Juhudi hizi zimepelekea pia udhibiti mkubwa wa magonjwa ya milipuko kama vile Kipindupindu na kuhara yaliyokuwa yanasababisha vifo vingi vya watoto nchini Haiti. Maboresho ya huduma bora ya maji safi na salama yanaendelea kwenye Kambi za watu wasiokuwa na makazi maalum.

Hizi ni juhudi zinazoonesha ushirikiano wa Mashirika ya Kimataifa pamoja na wadau mbali mbali wanaounganisha nguvu, rasilimali fedha na watu kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Haiti ambao waliathirika vibaya sana kutokana na tetemeko la ardhi lililoikumba nchi yao katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita na hivyo kupelekea maafa makubwa nchini humo.







All the contents on this site are copyrighted ©.