2013-01-11 11:20:03

Maandamano makubwa nchini Ufaransa kupinga muswada wa sheria kuhusu ndoa za watu wa jinsia moja!


Wanaharaki wanaotetea msingi bora wa maisha ya ndoa na familia kati ya Bwana na Bibi nchini Ufaransa, wanaendelea kujipanga kwa ajili ya kushiriki maandamano makubwa, Jumapili, tarehe 13 Januari 2013 dhidi ya sheria inayotaka kuhalalisha ndoa ya watu wa jinsia moja pamoja na kuwapatia fursa ya kuasi watoto. Hivi karibuni Serikali ya Ufaransa imeridhia muswada wa sheria unaojulikana kama "ndoa kwa wote" unaotoa mwanya hata kwa watu wa jinsia moja kuoana na kuishi unyumba kama Bwana na Bibi!

Waamini wa dini za Kikristo, Kiislam, Kiorthodox pamoja na Mashirika ya kutetea zawadi ya maisha bila kuwasahau wadau wa familia, wanatarajiwa kushiriki kwa wingi dhidi ya sheria hii inayodhalilisha utu na heshima ya binadamu, kwa kisingizio cha fursa na haki sawa za binadamu. Watu wote wamezaliwa kutokana na mapendo kati ya Bwana na Bibi; huu ndio ukweli unaowaunganisha wote. Ni changamoto kwa wananchi wa Ufaransa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu na mafao ya wengi kwa sasa na kwa siku za usoni.

Muswada wa sheria hii unapingana na maoni ya wananchi wengi nchini Ufaransa wanaopinga kwa dhati sheria inayotaka kuruhusu ndoa za watu wa jinsia moja, kwani ni kitendo ambacho ni kinyume kabisa cha ubinadamu na utu wema.







All the contents on this site are copyrighted ©.