Baba Mtakatifu Benedikto XVI kutoa Sakramenti ya Ubatizo kwa watoto wachanga, katika
maadhimisho ya Sherehe za Ubatizo wa Bwana
Monsinyo Guido Marini, mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa mjini Vatican anabaaianisha
kwamba, katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Ubatizo wa Bwana, hapo tarehe 13 Januari
2013, Siku kuu inayohitimisha Kipindi cha Noeli, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita, anatarajiwa kuwabatiza watoto ishirini katika Ibada itakayofanyika kwenye
Kikanisa cha Kipapa cha Sistina, kilichoko mjini Vatican. Hii ni kumbu
kumbu hai ya watoto hawa wanaozaliwa kwa Maji na Roho Mtakatifu, kama alivyofanya
Yesu mwenyewe alipobatizwa mtoni Yordani na hivyo kuyatakatifuza maji kuwa ni alama
ya kuzaliwa upya katika Roho Mtakatifu. Kwa njia ya Ubatizo wa toba, Yesu ambaye
hakuwa na dhambi, alionesha mshikamano wa dhati kabisa na binadamu anayeogelea katika
lindi la dhambi na mauti, ili aweze kumkirimia tena neema na baraka za kuwa mwana
mpendwa wa Mungu. Sakramenti ya Ubatizo kwa watoto hawa wachanga ni mlango wa kuingilia
katika maisha ya Kikristo, wakisaidiwa na wazazi pamoja na walezi wao wa Ubatizo.
Lakini Jumuiya ya waamini wanakumbushwa pia dhamana yao ya kusaidia malezi na makuzi
ya kiimani kwa watoto hawa. Katika Ibada ya Ubatizo, Baba Mtakatifu anatarajiwa
kusaidiwa na Askofu mkuu Giuseppe Sciacca, Katibu mkuu wa Mji wa Vatican pamoja na
Askofu mkuu Guido Pozzo, Mtunzaji mkuu wa Sadaka ya kitume. Ibada hii itafanyika kwenye
Altare ya Kanisa la Kipapa la Sistina kwa kuzingatia utajiri wake wa kisanaa. Baba
Mtakatifu wakati wa kubatiza atatumia simbi iliyonakishiwa, alama ya hija inayofanywa
na mwamini katika kuchuchumilia utakatifu na maisha ya uzima wa milele. Mwamini anapobatizwa
na kuingizwa katika Jumuiya ya waamini anaanza safari hii hatua kwa hatua katika maisha
yake kiimani.