2013-01-09 15:26:27

Yaliyojiri katika ziara ya Rais Kikwete Mkoani Tabora


Serikali, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, imetoa kwa makusudi, kandarasi ya mabilioni ya fedha kwa wakandarasi na wataalamu wengine wazalendo kwa nia ya kuunga mkono wanataaluma Watanzania na kuwapa nafasi kubwa zaidi katika kuchangia maendeleo ya nchi yao. Kandarasi hiyo ni ujenzi wa Daraja la Mto Mbutu, Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora daraja ambalo ujenzi wake utawanufaisha maelfu ya wananchi katika wilaya hiyo na wilaya za jirani za Iramba (Mkoa wa Singida), Meatu (Mkoa wa Simiyu) na Kishapu (Mkoa wa Shinyanga).

Kandarasi hiyo ina thamani ya Sh. Bilioni 11. 286 ya kazi ya usimamizi, ushauri na ujenzi wa daraja hilo utakuwa moja kwa moja kwa asilimia 100 mikononi mwa wataalamu Watanzania ambao wamekusanya nguvu zao kuweza kushinda kandarasi hiyo. Undani wa kandarasi hiyo ulitangazwa juzi, Jumapili, Januari 6, 2013, wakati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alipoweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Daraja hilo ambalo wataalam hao wazalendo wameahidi kuwa ujenzi wake utakamilika ifikapo Novemba, mwaka huu, 2013.

Miongoni mwa wataalamu hao wazalendo waliopewa kandarasi hiyo ni pamoja na makampuni 13 ya makandarasi, makampuni ya washauri na makampuni ya wasimamizi. Akizungumza kwenye sherehe hiyo, Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa John Pombe Magufuli alimwambia Rais Kikwete kuwa kandarasi hiyo imetolewa kwa wataalam wazalendo kulingana na ahadi ambayo Rais aliitoa wakati alipozungumza na wataalamu hao wakati wa kuadhimisha miaka 50 ya kuundwa kwa vyama vya kitaalamu vya sekta ya ujenzi mwaka juzi 2011.

“Mheshimiwa Rais, uliahidi kuunga mkono makandarasi wazalendo na kazi hii umeifanya. Tuna wakandarasi waliosajiliwa kiasi cha 9,447 kwa sasa nchini. Zamani walikuwa wanapata asilimia 30 ya miradi yote ya ujenzi nchini. Chini ya uongozi wako, sasa asilimia hiyo imepanda katika miaka ya uongozi wako hadi kufikia asilimia 50. Na sasa umetoa kandarasi hii. Tunakushuru sana.”

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Makandarasi nchini, Mhandisi Consolata Ngimbwa alimwambia Rais Kikwete katika sherehe hizo za uwekaji jiwe la msingi: “Haijawahi kutokea. Katika historia ya Tanzania, hakuna Rais aliyewahi kuwaamini watalaam wa nyumbani kwa kutoa kandarasi kubwa kiasi hiki kwa makandarasi wa nyumbani ama wataalam wengine wa Kitanzania. Tunakushukuru sana, sana Mheshimiwa Rais.”

Naye Rais Kikwete alisema: “Niliahidi kuwa Serikali ingewapa kazi, tena kazi kubwa. Lakini wakati huo niliwaambia kuwa kikwazo cha kupata kazi kubwa kilikuwa ni udogo wenu, kila mtu na lwake. Niliwaambia kuwa katika mambo haya kupiga uzalendo peke yake lilikuwa ni jambo halitoshi. Niliwaambia kuwa nguvu ya mnyonge ni umoja, Nashukuru kuwa mmelitambua hili na kujiunga katika umoja wenu. Dumisheni umoja huu.”

Aliongeza: “ Hii kazi tuliyowapa ni majaribio. Mkiweza kuifanya kazi hii vizuri basi utakuwa ni ufunguo wa kupata kazi nyingine. Hii ni flagship yenu.”

Wakati huo huo Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa Serikali yake inakaribia kukamilisha ujenzi wa madaraja yote 10 yaliyoahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 na ambayo yanagharimu mabilioni ya fedha. Rais Kikwete amesema kuwa kati ya madaraja hayo ambayo thamani yake inakaribia Sh. Bilioni 415, madaraja mawili tayari ujenzi wake umekamilika. Madaraja hayo ni lile la Ruhekei lililoko Wilaya ya Mbinga katika Mkoa wa Ruvuma na Daraja la Mwatisi katika Mkoa wa Morogoro.

Rais Kikwete amesema kuwa madaraja mengine saba yanaendelea kujengwa, ikiwa ni pamoja na Daraja la Kigamboni, Mkoa wa Dar es Salaam linalogharimu Sh. Bilioni 214.6, Daraja la Kikwete katika Mto Malagarasi, Mkoa wa Kigoma unaogharimu Sh. Bilioni 90.185, Daraja la Kilombero, Mkoa wa Morogoro linalogharimu Sh. Bilioni 53.214 na Daraja la Rusumo, Mkoa wa Kagera linalogharimu Sh. Bilioni 31.7.

Madaraja mengine yanayoendelea kujengwa ni Daraja la Sibiti, Singida, linalogharimu Sh. Bilioni 17.5, Daraja la Nangoo, Mkoa wa Mtwara linalogharimu Sh. Bilioni 4.29 na Daraja la Maligisu, Mwanza, linalogharimu Sh . Bilioni 2.51. Amesema Rais Kikwete: “Madaraja niliyotaja ujenzi wake ukikamilika, tutakuwa tumetimiza ahadi yetu ya kujenga madaraja yote yaliyotajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010 isipokuwa Daraja la Ruhuhu ambalo maandalizi yake ya ujenzi yanaendelea.”

Rais Kikwete alikuwa anazungumza wakati anaweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Mbutu, Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora katika sherehe ya kufana iliyofanyika Jumatatu, Januari 7, 2013. Amesema kuwa: “baadhi ya madaraja yanayojengwa sasa na Serikali yalipangwa kujengwa katika Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo mwaka 1968 lakini kwa bahati mabaya hayakuweza kujengwa. Madaraja hayo ni Daraja la Kigamboni, Daraja la Kirumi kwenye Mto Mara, Daraja la Rufiji, Daraja la Kilombero, Mkoa wa Morogoro na Daraja la Kikwete kwenye Mto Malagarasi. Awamu ya kwanza ya uongozi wa nchi yetu ilijenga Daraja la Kirumi kwenye Mto Mara, Awamu ya pili ikafanya maandalizi na Awamu ya tatu ikajenga Daraja la Rufiji na Awamu ya sasa inajega madaraja matatu yaliyobakia – Kilombero, Kigamboni na Kikwete.”

Daraja la Mbutu lina urefu wa kilomita tatu, na linajengwa katika Bonde la Mbutu na litaunganisha mikoa ya Tabora, Singida, Simiyu na Shinyanga.
Daraja hilo litakuwa na daraja moja kubwa la mita 60 na madaraja mengine madogo saba na hivyo kufanya urefu wa daraja lote kuwa na mita 165. Mpaka sasa asilimia 45 ya ujenzi wa daraja hili lenye thamani ya Sh. Bilioni 11.28 umekamilika na inakadiriwa kuwa litakuwa tayari ifikapo Novemba mwaka huu.

Rais Kikwete aweka jiwe la msingi kwa miradi ya kihistoria Tabora

Jumanne, Januari 8, 2013, imekuwa siku ya historia kwa Mkoa wa Tabora wakati maelfu ya wananchi wa Mkoa huo walipomshuhudia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete akiweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa barabara kubwa tatu za lami ambazo baadhi yake zinaunganisha Mkoa huo na mikoa mingine na ambazo ujenzi wake unagharimu mabilioni ya fedha za wananchi.
Barabara kubwa hizo ni za Nzega-Tabora, Tabora-Ndono hadi Urambo, na Tabora hadi Nyahua ambazo ujenzi wake unakadiriwa kugharimu kiasi kinachokaribia Sh. Bilioni 350 ambazo zote zinatolewa na Serikali ya Rais Kikwete. Rais Kikwete ambaye yuko katika ziara ya siku tano ya Mkoa wa Tabora kujionea mwenyewe jitihada za wananchi kujiletea maendeleo, ameanza siku yake ya jana kwa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Barabara ya Nzega-Puge-Tabora yenye urefu wa kilomita 115 katika sherehe iliyofanyika kwenye eneo la Puge kilomita 58.2 kutoka mjini Nzega kuelekea Tabora.

Barabara hiyo ambayo usanifu wake ulifanyika mwaka 2009 imegawanywa katika sehemu mbili za Nzega-Puge na Puge-Tabora na itagharimu jumla ya Sh. Bilioni 135, zikiwamo fedha ambazo zimetumika kufidia wananchi ambao wanaathiriwa na ujenzi wa Barabara hiyo.

Sehemu ya Nzega-Puge inagharimu Sh. Bilioni 66.36, inajengwa na kampuni ya CCCC ya China na itakamilika katika katika miezi 27 ijayo. Sehemu ya Puge-Tabora yenye urefu wa kilomita 56.8 inajengwa kwa gharama ya Sh. Bilioni 62.74 na Kampuni ya Sino Hydro ya China na itakuwa imekamilika katika miezi 26 ijayo.

Mradi mkubwa wa pili ambao Rais ameuwekea jiwe la msingi ni wa ujenzi wa Barabara ya Tabora-Ndono ambayo hata hivyo ujenzi wake utaendelezwa hadi kufikia mjini Urambo. Sherehe za uwekaji jiwe la msingi la Barabara hiyo iliyofanyiwa usanifu mwaka 2006 zimefanyika katika eneo la Mlolo, nje kidogo ya mji wa Tabora.

Barabara ya Tabora-Ndono yenye urefu wa kilomita 42 na inayojengwa na Kampuni ya Chico pia kutoka China kwa gharama ya Sh. Bilioni 51.34 na itamalizika katika kipindi cha miezi 20 kuanzia sasa. Gharama za mradi huo ni pamoja na Sh. Milioni 480 ambazo zimelipwa kwa wananchi kama fidia ya kupisha ujenzi wa barabara hiyo.

Barabara ya tatu kubwa ambayo Rais Kikwete ameiwekea jiwe la msingi ni ile ya Tabora hadi Nyahua yenye kilomita 85.6 na ambayo ujenzi wake unagharimu kiasi cha Sh. Bilioni 93.4. Ujenzi wa barabara hiyo unakadiriwa kumalizika mwanzoni mwa mwaka ujao 2014 na inajengwa na Kampuni ya CFTEC pia kutoka Jamhuri ya Watu wa China na sherehe zake za uwekaji jiwe la msingi zimefanyika katika eneo la Cheyo B, nje kidogo ya Mji wa Tabora.

Kwa Rais Kikwete kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo tatu, katika miezi michache ijayo na kwa mara ya kwanza Mji wa Tabora utakuwa umeunganishwa kwa barabara za lami kutoka kaskazini (tokea Nzega) kutoka magharibi (kutokea Urambo) na kutokea kusini (tokea Nyahua).

Ujenzi wa Barabara ya Nzega-Tabora kwa lami una maana kuwa makao makuu ya Mkoa wa Tabora sasa yanaunganishwa na Mkoa wa Shinyanga, ujenzi wa Barabara ya Tabora-Nyahua unalenga kuunganisha kwa lami Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Dodoma wakati Barabara ya Tabora-Ndono hadi Urambo na hadi Kaliua unaenda kuunganisha kwa lami Mkoa wa Tabora na ule wa Kigoma.

Aidha, ujenzi wa Tabora-Nyahua na Tabora-Ndono hadi Urambo na hatimaye Kaliua unalenga kujenga kilomita 700 za lami kutoka Manyoni, Mkoa wa Dodoma hadi Kigoma. Novemba 5, mwaka jana, 2012, Rais Kikwete aliweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya yenye kilomita 89.

Barabara hizo zote pia zinajengwa kulingana na ahadi ya Mheshimiwa Kikwete wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 na kwa sababu ya ukosefu wa wafadhili wa kuchangia gharama za ujenzi wa barabara hizo, fedha zote zinatolewa na Serikali ya Tanzania asilimia 100.








All the contents on this site are copyrighted ©.