2013-01-09 09:55:04

Kuna matumaini ya upatanisho wa kitaifa na ujenzi wa amani kwa wananchi wa Sudan


Mkutano kati ya Rais Omar Hassam el Bashir wa Sudan Kongwe pamoja na Rais Kiir Mayardit wa Sudan ya Kusini umepokelewa kwa hisia tofauti, baadhi ya watu wakionesha matumaini kwa wananchi wa Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini kuanza mchakato wa kujipatanisha, ili kujenga na kuimarisha amani na utulivu kama kikolezo cha maendeleo endelevu kwa kuheshimu na kuzingatia makubaliano yaliyokuwa yamekwishafikiwa kati ya Serikali hizi mbili, lakini yalikuwa hayajaanza kutekelezwa kwa vitendo.

Viongozi hawa wameamua kudumisha amani, kuanza tena uzalishaji wa petroli kutoka Kusini mwa Sudan na inayosafirishwa hadi Khartoum. Kwa kipindi cha mwaka mzima, Serikali ya Sudan ya Kusini ilisimamisha uzalishaji wa Petroli, hali ambayo ilileta athari kubwa kwa uchumi wa mataifa haya mawili, kwani pato kubwa la taifa linategemea uzalishaji wa Petroli. Uzalishaji wa mafuta unagusa pia uchumi wa Makampuni ya Kimataifa ambayo yamewekeza katika nishati hii.

Rais Mwai Kibaki wa Kenya ameonesha kuridhika kwake na maamuzi yaliyofikiwa na viongozi wa nchi mbili hizi, chini ya usuluhishi uliofanywa na Rais mstaafu wa Afrika ya Kusini, Thabo Mbeki. Kenya inapenda kuwahakikishia wananchi wa Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini, kwamba, itaendelea kuunga mkono juhudi za nchi hizi mbili kudumisha amani na utulivu kwa ajili ya mafao ya wengi, ndiyo maana Serikali ya Kenya ilijihusisha kikamilifu katika mchakato wa kutafuta usalama, amani na utulivu kwa wananchi wa Sudan.

Sasa ni wakati wa kujikita zaidi katika kuanza mchakato wa upatanisho wa kitaifa, ili amani ya kudumu iweze kupatikana.







All the contents on this site are copyrighted ©.