Katekesi ya Papa kwa mahujaji na wageni - yatafakari fumbo la Umwilisho wa Mungu.
Baba Mtakatifu Benedikto XV1, katika mafundisho yake ya Jumatano hii kwa mahujaji
na wageni, ameangalisha katika sherehe za kipindi hiki cha Noel, ambamo Kanisa linaendelea
kutafakari fumbo kuu la Mungu , aliyeshuka chini toka Mbinguni na kuingia katika
ubinadamu wetu. Siri ya Yesu Kristu, Mwana wa Mungu aliyemwilishwa na kuwa binadamu
kama sisi, na kwa namna hiyo , aliifungua njia ya inayotuelekeza mbinguni, kupitia
usharika kamili nae.
Katika siku hizi , Papa anasema, Makanisa yote kwa mara
ingine, yanatafakari maana ya nafsi ya Mungu kumwilishwa,kama inavyodhihirishwa
na uhalisi wa Siku Kuu ya Noel. Mungu anashuka duniani katika hali ya binadamu, kama
tunavyokiri katika sala ya Nasadiki, msingi wa Imani ya Mkristu. Katika maelezo
yake Papa alitazamisha hasa katika maana ya neno hili umwilisho, kiini cha Imani
ya Kikristu. Maelezo ya Papa juu ya siri hii ya Mwana wa Mungu aliyefanyika mwili
yametazamishwa katika maandiko mengi Matakatifu (Yn 01:14), na pia nyaraka za Mababa
na walimu wa kanisa wa tangu mwanzo wa Kanisa, akitaja baadhi yao kama Mtakatifu
Ignazio wa Antiokia, MtaktAifu Ireneo, waliotumia sana, Injili ya Mtakatifu Yohane,
kueleza maana na Neno aliyefanywa kuwa mwili. Na hivyo, Neno mwili kwa maenezo ya
Kiebrania linaonyesha ubinadamu ulioshikanishwa na utu wa mtu katika hali zake zote
za udhaifu na uhalisia.
Ndiyo kusema, kwamba wokovu uliotoka kwa Mungu, kwanza
ulikuwa Neno, na Neno likafanywa kuwa mwili, nalo ni Yesu wa Nazareti, aliyezaliwa
kama binadamu na kuyaishi maisha yetu kama kibinadamu katika hali zote alimojikuta,
kwa ajili ya wokovu wetu, na ili sisi tupate kuwa, katika Yeye, wana warithi wa Baba
yetu wa mbinguni.
Katika Mtoto wa Bethlehemu, Mungu alitupatia zawadi kubwa
kuliko zote, zawadi ya nafsi yake. Kwa ajili yetu, Mungu akawa mmoja wetu na kuushiriki
ubinadamu wetu kikamilifu, akituwezesha kubadilishana nae hisia za maisha yake mwenyewe
ya Kimungu. Hii ni siri kubwa yenye kuonyesha ukweli na kina cha upendo wa Mungu kwetu.
Papa ameutaja pia kuwa ni mwaliko unaotuhumiza kutoa jibu kwake yeye kwa imani,
kuukubali ukweli wa neno lake linalo yatengeneza upya maisha yetu kila siku. Katika
kutafakari fumbo la Umwilisho, tunamwona Kristo , Adamu mpya, mtu mkamilifu anaye
zindua uumbaji mpya, na kuirejesha sura yetu ya kufanana na Mungu na kuionyesha hadhi
ya ubinadamu na utu wetu (taz. Gaudium et Spes, 22). Papa alimalizia kwa kusema,
tunapoendelea kutafakari juu ya fumbo hili kuu katika siku hizi za mwisho wa kipindi
cha Noel, na tufurahi zaidi na zaidi katika mwanga wa Utukufu wa Bwana, unaotuwezesha
daima kuimarika na kufanana na Mwana wa Mungu aliye mwilishwa na kuwa binadamu kama
sisi.