Jicho la Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa Bara la Afrika 2013
Hotuba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, hapo tarehe 7 Januari 2013, kwa
Mabalozi na wawakilishi wa nchi, Umoja wa Ulaya na Mashirika ya Kimataifa 179 yenye
uhusiano wa Kidiplomasia na Vatican, imeliangalia pia Bara la Afrika kwa jicho la
pekee kabisa, akizitaka hata nchi za Afrika ya Kaskazini kutoa kipaumbele cha pekee
kwa raia wake wote; kwa kushirikiana nao pamoja na kuwahakikishia uhuru wa kidini
unaowapatia fursa ya kuiungama imani yao hadharani pamoja na kuchangia mafao ya wengi.
Baba
Mtakatifu katika salam na matashi mema kwa Mwaka Mpya wa 2013, ametumia fursa hii
kuwahakikishia wananchi wa Misri uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala na sadaka yake
wakati huu Misri inapoendelea na mchakato wa mabadiliko makubwa kwa taasisi mbali
mbali nchini humo.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akiyaelekeza
macho yake Kusini mwa Jangwa la Sahara, anasema kwamba, anaendelea kuunga mkono juhudi
za ujenzi wa amani hasa katika zile nchi ambazo bado zina majeraha ya vita, kinzani
na misigano ya kidini na kijamii, mambo yanayoendelea kuleta maafa makubwa kwa Jamii.
Baba Mtakatifu amegusia kwa namna ya pekee, Nchi zilizoko kwenye Pwani ya
Pembe ya Afrika, DRC na baadhi ya Nchi za Kiafrika ambazo, machafuko yanaendelea kusikika
siku hadi siku, kiasi cha kuwafanya baadhi ya watu kuyakimbia makazi, familia na hali
halisi ya maisha yao.
Nigeria imekuwa ni nchi ambayo vitendo vya kigaidi vinaendelea
kutawala siku hadi siku, kiasi kwamba, watu hawana uhakika na usalama wa maisha na
mali zao. Inasikitisha kuona kwamba, vitendo hivi vya kigaidi vinafanywa dhidi ya
Wakristo wanapokuwa wakisali, hali inayoonesha chuki na uhasama wa kidini, badala
ya kujenga na kuimarisha amani na mshikamano wa kitaifa; watu wanajenga hofu na woga.
Matukio ambayo yamejirudia hata wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka
2012, Wakristo kadhaa nchini Nigeria waliuwawa kikatili.
Nchi ya Mali inaendelea
kukumbwa na vita, kinzani na migogoro ya kisiasa na kijamii, jambo ambalo linahitaji
Jumuiya ya Kimataifa kuingilia kati ili kuokoa maisha ya watu na kwamba, juhudi za
majadiliano kati ya viongozi wakuu wa mgogoro huu zilete matunda ya amani ya kudumu,
vinginevyo, Mali itajikuta ikitumbukia katika vita ya wenyewe kwa wenyewe.