Watu 9 wafa maji Ziwa Tanganyika, wengine 12 hawajulikani waliko!
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania, ametuma salamu za rambirambi kwa Mkuu wa Mkoa
wa Kigoma, Mheshimiwa Issa Machibya kuomboleza vifo vya watu tisa katika ajali ya
kuzama kwa boti katika Ziwa Tanganyika iliyotokea juzi na ambako mpaka sasa watu wengine
12 waliokuwamo kwenye boti hiyo hawajulikani walipo.
Katika salamu zake za
rambirambi alizotoa, Jumamosi, Januari 5, 2013, Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa
Machibya, “Nimepokea kwa mshtuko mkubwa na huzuni nyingi taarifa za vifo vya watu
tisa waliopoteza maisha katika ajali ya kuzama kwa boti iliyokuwa inasafiri katika
Ziwa Tanganyika kutoka Kigoma kwenda nchi jirani ya Burundi. Aidha, nimejawa na wasiwasi
kutokana na taarifa kuwa watu wengine 12 waliokuwepo katika boti hiyo hawajulikana
walipo.”
“Nakutumia wewe Mkuu wa Mkoa wa Kigoma salamu za rambirambi za dhati
ya moyo wangu kutokana na ajali hiyo na upotevu huo wa maisha. Aidha, kupitia kwako
nazitumia salamu zangu za rambirambi familia zote ambazo zimepoteza wapendwa wao katika
ajali hiyo. Wajulishe kuwa niko nao katika kipindi hiki kigumu cha machungu ya kupotelewa
na ndugu zao. Kwa wale ambao mpaka sasa hawajui ndugu zao wako wapi nawaombea subira
na uvumilivu wakati jitihada zinafanyika kuwatafuta.”
Ameongeza Mheshimiwa
Rais: “Aidha, napenda kupitia kwako Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa niwajulishe wafiwa wote
kuwa nawaombea uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu. Naungana nao katika
kumwomba Mwenyezi Mkuu, Mwingi wa Rehema aziweke pema peponi roho za marehemu.”
Katika
salamu zake, Rais Kikwete pia amewaombea wote walioumia katika ajali hiyo wapata ahueni
ya haraka ili waweze kurejea kwenye shughuli zao za kujitafutia maendeleo.