Ghasia za kidini Tanzania zinamnyima usingizi Rais JK
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amewataka viongozi wa dini zote nchini kufufua
ama kuhuisha na kutumia ipasavyo mawasiliano mazuri yaliyokuwepo miaka ya nyuma baina
ya viongozi wa dini zote nchini kama njia ya kuliepusha taifa na majanga yanayoweza
kuhatarisha amani kupitia ghasia za kidini.
Aidha, Rais Kikwete ametaka kujengekeza
zaidi kwa utamaduni wa kuheshimiana na kuvumiliana baina ya watu wa dini na madhehebu
mbali mbali nchini kwa sababu ni dhahiri kuwa zipo dalili za kupungua kuheshimiana
na kuvumiliana kwa misingi ya tofauti za dini.
Rais pia amesisitiza kuwa viongozi
wa dini na viongozi wa Serikali wote wanao wajibu uliosawa ambao ni kuwaendeleza wananchi
hata kama kwa njia tofauti – kundi moja likiifanya kazi hiyo kwa njia ya kiroho na
kundi jingine kwa njia ya maendeleo. Serikali yake itaendelea kulinda uhuru wa wananchi
kuabudu kwa sababu haki hiyo ni msingi muhimu na inayochangia amani na utulivu katika
Tanzania.
Rais Kikwete ameyasema hayo Jumapili, Januari 6, 2013, wakati alipozungumza
kwenye Sherehe za Kuwekwa Wakfu na Kusimikwa kwa Askofu Mteule Dkt. Alex Seif Mkumbo
kuwa Askofu wa Dayosisi ya Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT)
kwenye Kanisa Kuu Imanuel, mjini Singida.
Amewaambia mamia kwa mamia ya waumini
na viongozi mbali mbali wa dini na Serikali: “Miaka ya nyuma kulikuwa na utaratibu
nzuri wa mawasiliano ya karibu baina ya viongozi wa dini zote hapa nchini. Viongozi
wetu walikuwa wanakutana mara kwa mara kuzungumzia masuala mbali mbali yenye maslahi
kwa dini zao na waumini wao na kwa nchi yetu kwa jumla. Walitumia vikao hivyo kujadili
masuala yenye matatizo na tofauti baina yao na kuyapatia majawabu.”
Ameongeza
Rais Kikwete: “Hii ilisaidia kuwepo kwa maelewano na utulivu tuliokuwa nao kwa muda
mwingi. Naamini tunauhitaji sana utaratibu huu nzuri sasa kuliko wakati mwingine.
Naomba ufufuliwe kama ulikufa au uhuishwe kama umesinzia. Na kubwa zaidi utumike ipasavyo.Nchi
yetu inapitia kipindi kigumu, hivyo utaratibu huu utaliepusha taifa letu na madhara
yanayoweza kuhatarisha amani na utulivu. Itatundolea sisi Serikali ulazima wa kutumia
vyombo vya dola kulinda amani na kutuliza ghasia.”
Kuhusu utamaduni wa kuheshimiana
na kuvumiliana kwa misingi ya dini, Rais Kikwete amesema: “Napata hofu sana ninapoona
dalili za kupungua kuheshimiana na kuvumiliana kwa tofauti zetu hasa kwa upande wa
dini. Mwaka 2012 ulikithiri kwa vitendo na matukio hayo. Nashukuru Mungu juhudi za
pamoja za viongozi wa dini na Serikali ziliweza kuzuia mambo kutokuwa mabaya zaidi.
Juhudi hizi lazima ziendelee ili mambo hayo yasitokee tena na hali ya kutiliana mashaka
na chuki viondoke kabisa miongoni mwa waumini na wafuasi wa dini na madhehebu mbali
mbali.”
Rais Kikwete pia amewahakikishia wananchi wa Mkoa wa Singida kuwa Serikali
yake haijasahau kujenga uwanja wa ndege wa mjini Singida. “Shabaha yetu ni kujenga
uwanja wa urefu wa kilomita mbili ili kuwezesha ndege za abiria 70 kutua. Usanifu
utafanyika mwaka huu kisha tuanze ujenzi.”