2013-01-04 09:32:39

Miaka 10 baada ya Mauaji ya Askofu mkuu Michael Aiden Courtney, Balozi wa Vatican nchini Burundi, wahusika hawajatiwa bado mbaroni!


Kanisa Katoliki Burundi linafanya kumbu kumbu ya miaka kumi tangu Askofu mkuu Michael Aiden Courtney, Balozi wa Vatican nchini Burundi, alipouwawa kikatili na watu wasiojulikana, hapo tarehe 29 Desemba 2003, hadi leo hii hakuna yeyote aliyetiwa mbaroni kuhusiana na mauaji haya. Miaka mitatu iliyopita, Baraza la Maaskofu Katoliki Burundi lilitangaza kwamba, kila Mwaka ifikapo tarehe 29 Desemba, itakuwa ni Siku maalum kwa ajili ya kuombea amani na upatanisho wa kitaifa.

Katika mahubiri yake, Askofu Venant Bacinon wa Jimbo Katoliki Bururi, amemkumbuka Hayati Askofu mkuu Courtney kuwa ni mtu aliyesimama kidete kutangaza Injili ya Amani inayopata chimbuko lake katika majadiliano ya kweli, ili kujenga msingi wa umoja wa kitaifa kwa wananchi wa Burundi baada ya mauaji ya kimbari yaliyofanyika kunako mwaka 1993. Wananchi wa Burundi wanahamasishwa kupenda, kuheshimu na kutunza zawadi ya uhai.

Kumbu kumbu ya miaka kumi tangu Askofu mkuu Courtney alipouwawa kikatili iwe ni fursa ya kuchuchumilia misingi ya haki, amani na upatanisho nchini Burundi. Serikali inawajibu wa kuhakikisha kwamba, inawatia mbaroni watu waliohusika na mauaji ya Askofu mkuu Courtney ili haki iweze kutendeka.

Kwa upande wake Askofu mkuu Franco Coppola, Balozi wa Vatican nchini Burundi anabainisha kwamba, amani ndiyo njia pekee itakayoweza kukoleza na kudumisha maendeleo ya wananchi kiroho na kimwili, sanjari na kujenga msingi wa umoja na upatanisho wa kitaifa. Hakuna maendeleo ya kweli pasi na amani anasema Askofu mkuu Coppola.

Parokia ya Minago imeomba kujenga shule ya Sekondari kama kumbu kumbu endelevu ya uwepo wa Hayati Askofu Courtney miongoni mwao, ili kufundisha pamoja na mambo mengine, elimu ya amani na upatanisho, ili kuwawezesha watu wengi zaidi kujitosa kutangaza Injili ya Amani kama alivyobainisha Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili. Amani, umoja na upatanisho ni fadhila ambazo Askofu mkuu Courtney alizipigania katika utume wake wa kichungaji nchini Burundi.







All the contents on this site are copyrighted ©.