2013-01-04 07:26:06

Majandokasisi wanne kupewa daraja takatifu la Ushemasi Jimboni Dodoma


Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma, katika maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, hapo tarehe 6 Januari 2013 anatarajiwa kutoa daraja takatifu la Ushemasi kwa Majandokasisi wane wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, katika Ibada ya Misa Takatifu itakayofanyika kwenye nyumba ya malezi, Miyuji, Dodoma. RealAudioMP3

Mashemasi watarajiwa ni Alex Issengwa, Danford Mhaumi, John Greyson na Raymond Kaele. Kabla ya kupewa daraja la Ushemasi, Majandokasisi hao watapokelewa rasmi katika Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, hapo tarehe 5 Januari 2013. Ibada hii itaongozwa na Mheshimiwa Padre Reginald Mrosso, C.PP.S, Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania.

Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania lina jumla ya Wamissionari 69 wanaofanya kazi za kitume nchini Tanzania, Guinea Bissau, Italia, Marekani na Colombia, hali inayoonesha kukua na kukomaa kwa Shirika hili nchini Tanzania; matunda ya Mtaguso mkuu wa pili wa Vatican na changamoto ya ari na moyo wa kimissionari.

Kupokelewa kwa Mafrateri hao wane, kutaifanya idadi ya Wamissionari hao kufikia 73, hata hivyo, Shirika linaendelea kuwahamasisha waamini kutambua kwamba, mavuno ni mengi, lakini watenda kazi katika shamba la Bwana ni wachache, kumbe wanao wajibu wa kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea miito pamoja na kutambua kwamba Familia za Kikristo ni kitalu cha kuzalisha, kukuza na kulea miito.

Wazazi watekeleze wajibu wao kikamilifu katika kurithisha imani, maadili na tunu bora za kiutu, ili Kanisa liweze kupata watenda kazi mahiri, watakatifu na wachamungu, watakaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kumtumikia Mungu na jirani zao sanjari na ujenzi wa Ufalme wa Mungu hapa duniani.

Waamini waendelee kuwasindikiza makleri katika sala ili watekeleze majukumu yao wakiwa na ari na ule mwamko waliokuwa nao tangu awali walipoamua kujitoa kwa ajili ya maisha na utume wa Kipadre na kamwe wasikate tama wala kukengeuka wakiwa njiani.








All the contents on this site are copyrighted ©.