2013-01-02 10:19:19

Kardinali Pengo asema: utu na heshima ya binadamu visaidie kujenga na kuimarisha amani duniani


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, tarehe Mosi, Januari 2013, Siku ya Kuombea Amani Duniani amesema kwamba, wajenzi wa amani ni watoto wa Mungu, wanaojitahidi kushinda ubaya kwa kutenda mema, wakitumia nguvu ya ukweli; silaha ya sala na msamaha. Ni watu wanaofanya kazi halali kwa juhudi, bidii na maarifa.

Tafiti zao za kisayansi zinalenga zaidi katika mafao ya binadamu wengi; ni watu wanaomwilisha Injili ya Upendo katika matendo ya huruma: kiroho na kimwili. Itakumbukwa kwamba, ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa Siku ya 49 ya Kuombea Amani Duniani ulikuwa unaongozwa na kauli mbiu "heri wapatanishi".

Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, katika Salam zake za Mkesha wa Mwaka Mpya 2013, uliofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu la Dar es Salaam, amewataka watanzania kuhakikisha kwamba, wanatoa kipaumbele cha kwanza katika kutafuta, kulinda na kudumisha misingi ya amani ambayo imekuwa ni dira na mwongozo wa watanzania kwa miaka mingi; lakini amani hii inaanza kupotea taratibu.

Watanzania wajenge utamaduni wa kuheshimu na kuthamini utu na heshima ya kila mtu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Imani za kidini zisiwe ni chanzo cha kinzani na migogoro ndani ya Jamii, bali ziwasaidie kudumisha upendo na mshikamano wa kitaifa. Amani na utulivu ni jambo muhimu sana katika maisha na maendeleo ya watu.

Watanzania wafanye tafakari ya kina kuangalia mambo yaliyohatarisha amani, usalama na utulivu miongoni mwao, ili matukio hayo yasijirudie tena. Vitendo vya uchomaji wa Makanisa pamoja na Padre Ambrose Mkenda wa Jimbo Katoliki Zanzibar kupigwa risasi wakati wa Noeli ni matukio ambayo yanahatarisha amani, usalama na utulivu miongoni mwa watanzania. Amani ni jambo la msingi ambalo kamwe halipaswi kuchezewa!







All the contents on this site are copyrighted ©.