2013-01-01 12:30:17

Wajenzi wa amani ni wale wanaojitahidi kushinda ubaya kwa wema; wakitumia nguvu ya ukweli, silaha ya sala na msamaha; kwa kazi halali na makini na kwa ajili ya wengi!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumanne, tarehe Mosi, Januari 2013 amewatakia watu wote heri na baraka kwa Mwaka Mpya wa 2013: Bwana awabariki na kuwalinda, awaangazie nuru ya uso wake na kuwafadhili; Bwana awainulie uso wake na kuwapatia amani.

Hii ndiyo baraka ya Mwaka Mpya inayopata chimbuko lake kutoka katika nuru ya uso wa Mungu uliomfikia mwanadamu kwa njia ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo, katika hali ya unyenyekevu na maficho makubwa kule mjini Bethlehemu. Bikira Maria, Mtakatifu Yosefu na baadhi ya wachungaji ndio waliofanikiwa kuuona ufunuo huu na baadaye mwanga wa Kristo umeweza kuonekana na watu wengi wa Mataifa. Mara kwanza, mwanga huu uliojionesha katika Nchi Takatifu na kwa njia ya Roho Mtakatifu Injili ya Amani imeweza kuwafikia watu wengi zaidi.

Utukufu kwa Mungu juu na amani duniani kwa watu wenye mapenzi mema, ni wimbo wa Malaika na Wakristo wakati wa Kipindi cha Noeli unaobubujika upendo unaopania kujenga majadiliano, uelewano na upatanisho. Kanisa linaonesha kuzaliwa kwa Yesu Kristo, Mfalme wa Amani, sanjari na kuadhimisha Siku ya Kuombea Amani Duniani, kwa kutambua kwamba, wajenzi wa amani ni watoto wa Mungu.

Ni watu wanaojitahidi kushinda ubaya kwa kutenda mema, wakitumia nguvu ya ukweli, silaha ya sala na msamaha; kwa njia ya kazi halali inayotekelezwa kwa umakini mkubwa; kwa tafiti za kisayansi zinazolenga mafao ya binadamu; kwa matendo ya huruma: kiroho na kimwili. Kuna wajenzi wengi wa amani, lakini wanatekeleza majukumu yao katika hali ya ukimya, lakini wanachachusha ubinadamu mintarafu Mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, Mwaka Mpya ni kama safari, kwa njia ya mwanga na neema ya Mungu uwawezeshe watu kuanza hija ya amani kwa kila mtu, familia, mahali na ulimwengu mzima, wakijitahidi kuupokea na kuukumbatia upendo wa Kristo. Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu amemtakia kheri na baraka Rais Giorgio Napolitano wa Italia pamoja na viongozi mbali mbali waliomtumia salam na matashi mema katika Mwaka 2013.

Amewashukuru vijana wa kiekumene wa Jumuiya ya Taizè wanaohudhuria mkutano wa thelathini na tano wa sala hapa Roma. Amewashukuru waamini na vikundi mbali mbali vilivyojitahidi kuandaa matukio mbali mbali kwa ajili ya kuenzi Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.