Zaburi hii ni kilio cha anayeonewa. Muhusika ni yeye mwenyewe au mwakilishi wa wengine.
Maisha yake yapo katika hatari kutokana na watu wanaomzunguka na ambao mwanzoni walikuwa
rafiki zake. Leo hii wimbo huu waweza kuimbwa na yeyote kati yetu anayetambua kwamba
anaonewa.
Anaanza kwa kumwita Mungu ajitokeze kama shujaa: Uishike ngao na
kigao. Inaonekana mtunzi na wenzake wamegeuka wakimbizi milimani, kutokana na kuwahofia
watesi wao. Maadui hawa wapo kila mahali: mahakamani ni washitaki wao, maadui zao
vitani, ni wawindaji wanaotupa nyavu na kuchimba mashimo kuwatega, ni majambazi mitaani,
ni wanyama wakali mwituni. Watesi hawa wanavumisha matusi na maneno ya kejeli kwao,
kote kote hatari inawazunguka. Shaka yake anaieleza kwa hemo la kukata tamaa: Bwana,
hata lini utatazama?
Mtunzi wetu picha anayotuchorea ni kuwa ni mtu mwadilifu
na mpole anayefuata nyendo za baba zake. Anachoomba ni kuwa yeye na wenzake waachwe
huru. Kwa kutumia kanuni ya jino kwa jino, anawaombea watesi wao wapate fadhila kama
wanayowapatia wao.
Tunafundishwa naye jinsi ya kuwafariji watu wenye huzuni,
kwani hata yeye ameonja huzuni. Tunapaswa kuhuzunika na wenye kuhuzunika, huzuni ya
kweli na si ya mamba. Mtu mmoja alikuwa na uchungu mkubwa na kuuliwa kinyama kwa mtoto
wake mpenzi. Wakati wa ibada ya maziko, mwongoza ibada alipotoa chozi kutokana na
ukatili huo, mzazi wa mtoto huyo, moyo wake ukafunguka kwa tulizo la amani. Tukumbuke
“Heri walio na huzuni, maana hao watatulizwa” (Mt 5:4).
Mtunzi anaahidi kama
ataokolewa toka katika midomo ya simba, ataenda mbele ya kusanyiko kumtolea Bwana
sifa ya shukrani. Tunakumbushwa kuwa nasi tu viungo katika mwili wa Kristo, na tunapopata
fadhila fulani tusikose kuwashirikisha wengine furaha yetu.
Maneno Ewe! Ewe!
Jicho letu limeona! Ni msemo wenye kuonesha dharau toka kwa wajinga ambao wamemwinukia
mteswa wetu. Leo hii tunaweza kuyaweka katika msemo mmoja, mteswa wetu anaambiwa ‘amefulia.’
Mbaya zaidi, alisingiziwa mengi na mashahidi wa uongo walijitokeza dhidi yake. Hali
hii ndiyo iliyompata Yesu wa Nazarethi (soma Mt 26:57-62).
Kwa jitihada kubwa
anamsihi Bwana ‘umeona,’ ‘usiwe mbali,’ ‘amka’ ili amsaidie. Tunakumbushwa naye jukumu
letu la kukumbuka kuwa watu wa shukrani kwa wale waliokuwa nasi tulipokuwa katika
shida, iwe ya binafsi au ya taifa. Kwa namna ya pekee anahitimisha kwa kubainisha
kwamba wakishinda shida yao, hawatajisifu wenyewe, bali waukumbuka mkono mwema wa
Mungu kwa shukrani!