2012-12-31 07:58:19

Mwaka 2013 ni Mwaka wa Mshikamano wa Kimataifa


Utukufu kwa Mungu juu na amani duniani kwa watu wenye mapenzi mema ni ujumbe unaoendelea kusikika masikioni mwa mwengi wakati huu wa maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, lakini kwa bahati mbaya dunia bado inaendelea kushuhudia vita, migogoro na kinzani za kijamii. Fumbo la Umwilisho linapata utimilifu wake katika Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo.

Mwenyezi Mungu ameweza kuupatanisha ulimwengu pamoja naye; changamoto kwa binadamu kuendelea kujipatanisha wao kwa wao, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi, kwani bado chuki na uhasama vinaendelea kutawala katika mioyo ya watu na kwamba, amani ya kweli inaonekana kuwa mbali kutokana na misimamo mikali ya kiimani pamoja na uchu wa mali na madaraka.

Imekwishagota miaka 1700, tangu Mfalme Costantino mkuu alipotoa ruhusa ya uhuru wa kidini kwa watu wote kwa Tamko la Milano, kunako mwaka 313 Baada ya Kristo, bado kumekuwepo kwa madhulumu ya kidini na waathirika wengi ni waamini wa dini ya Kikristo kama takwimu zinavyonesha kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Hii ni sehemu ya ujumbe wa Kipindi cha Noeli uliotolewa na Patriaki Bartolomeo wa kwanza kwa Kanisa Kiorthodox la Costantinopoli kwa waamini wa Kanisa lake pamoja na watu wote wenye mapenzi mema. Anasema, athari za myumbo wa uchumi kimataifa ni matokeo ya ubinafsi, uchoyo pamoja na kukumbatia uchumi wa kibepari unaongalia mtaji na faida kubwa hata kwa gharama ya maisha ya watu wengi.

Hizi ni dalili za kumong’onyoka kwa maadili na utu wema na watu wanadhani kwamba, soko huria lisilozingatia maadili, sheria na kanuni za fedha ni mkombozi wa uchumi na soko la dunia. Lakini hii ni ndoto inayoendelea kuwatumbukiza watu wengi katika umaskini wa kipato na ki hali sanjari na vitendo vya jinai vinavyovuka mipaka ya kitaifa na kimataifa. Matukio yote haya ni hatari kwa amani na usalama wa Jumuiya ya Kimataifa.

Kanisa la Kiorthodox linaendelea kufuatilia matukio mbali mbali ya vita, kinzani za kijamii, kisiasa na kimaadili pamoja na maafa asilia mambo ambayo yanatoa changamoto kubwa kwa waamini kujikita katika mshikamano wa upendo, kwa kuwafariji na kuwasaidia jirani wanaoteseka kutokana na hali ngumu ya maisha.

Ndiyo maana Kanisa la Kiorthodox linautangaza Mwaka 2013 kuwa ni Mwaka wa Mshikamano Kimataifa. Lengo ni kushikamana katika mapambano dhidi ya umaskini na baa la njaa linaloendelea kutesa mamillioni ya watu duniani sanjari na kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya: haki, amani, usawa.

Patriaki Bartolomeo wa kwanza anahitimisha ujumbe wake wa Noeli kwa kusema kuwa, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili na kuzaliwa na Bikira Maria kwa njia ya Roho Mtakatifu ndiye Mkombozi wa dunia na Mfalme wa Amani, asaidie juhudi za mshikamano wa kimataifa, uhuru, upatanisho, amani na matashi mema miongoni mwa watu. Awe ni chemchemi ya uvumilivu, matumaini na nguvu thabiti.









All the contents on this site are copyrighted ©.