2012-12-31 08:02:13

Familia inajukumu la kurithisha imani, kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli!


Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, Familia kimsingi inapaswa kuwa ni shule ya utakatifu, haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. RealAudioMP3

Hapa ni mahali ambapo watu wanajifunza tunu bora za maisha ya kijamii, kiutu na kimaadili. Huu ndio wajibu msingi wa wazazi na walezi katika familia, kiasi cha kuwafanya kuwa ni wajenzi wa tunu hizi katika jamii inayowazunguka.

Lakini kwa bahati mbaya, mambo sivyo yanavyokwenda katika hali halisi ya familia nyingi sehemu mbali mbali za dunia. Hii inatokana na changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia bila kusahau tabia ya ukanimungu inayopelekea watu wengi kumezwa na malimwengu kiasi hata cha kusahau wajibu na dhamana ya familia ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.

Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, kuna baadhi ya familia zimeshindwa kurithisha tunu bora za maisha ya kijamii, kiutu na kimaadili na matokeo yake dunia inakuwa ni uwanja wa fujo na vurugu. Baadhi ya wazazi wamechangia kuporomoka kwa tunu msingi za maisha ya kifamilia na hivyo familia inakosa ile dhamana ya kuwa ni shule ya utakatifu, haki na amani kama ambavyo ingetarajiwa kuwa!

Baadhi ya wazazi wanawafundisha watoto wao kudharau na kubeza dini na imani za watu wengine ndani ya Jamii, jambo ambalo ni hatari kubwa kwani ndiyo chanzo cha kinzani na migogoro ya kidini inayoendelea kufuka moto sehemu mbali mbali za Bara la Afrika na duniani kwa ujumla. Familia zisipotekeleza wajibu wake barabara, kuna hatari kubwa kwamba, misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli itakuwa daima hatarini. Familia zijengewe uwezo wa kurithisha tunu bora za maisha ya kijamii, kiutu na kimaadili, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Askofu mkuu Josephat Lebulu anasema kwamba, Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu iwe ni mfano na kielelezo makini cha utekelezaji wa dhamana na majukumu ya kifamilia kwa kujikita katika kufanya kazi kwa juhudi, bidii na maarifa; sala, kusoma na kulitafakari Neno la Mungu, kujitajirisha kwa neema na Baraka za Mwenyezi Mungu kwa njia ya maisha ya Kisakramenti pamoja na kumwilisha Imani katika matendo.

Jukumu kubwa la Familia za Kikristo wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani ni kuhakikisha kwamba, Familia zinakuwa ni chemchemi za kurithisha imani tendaji kwa watoto wao.








All the contents on this site are copyrighted ©.