Uzinduzi wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani: Shirika la Wamissionari wa Damu Takatifu
ya Yesu, Tanzania
Wamissionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, tarehe 29 Desemba
2012 wamezindua rasmi Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Kanda ya Manyoni, Jimbo Katoliki
Singida, kwa kuzihusisha Parokia za Chibumagwa, Manyoni na Itigi. Walengwa wakuu ni
Wanashirika pamoja na waamini wa Parokia zinazohudumiwa na Wamissionari hao, Jimbo
Katoliki Singida.
Mwaka wa Imani unakwenda sanjari pia na Maadhimisho ya Miaka
200 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, kunako tarehe
15 Agosti 1815. Vikarieti ya Tanzania inajiandaa pia kuwa ni Kanda kamili ifikapo
mwaka 2015, kama kielelezo cha ukomavu wa imani na huduma kwa Familia ya Mungu katika
maeneo wanayohudumia. Ifuatayo ni tafakari iliyotolewa na Mheshimiwa Padre Reginald
Mrosso, C.PP.S, Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu katika uzinduzi
huu.
Mwaka huu wa Imani unamwalika kila mbatizwa: Kukiri
imani ya kweli na kuishi imani hiyo kila siku ya maisha. Kumtangaza Yesu au kuinjilisha
kwa maneno na vitendo, kwa hali na mali. Kuimarisha maisha mema ya Kikristu katika
familia, JNNK, parokia na pote. Kumtafuta Yesu kwa dhati na kujenga uhusiano wa
karibu na wa kudumu naye Kuimarisha moyo wa sala, maisha ya sakramenti na tafakari
ya Neno la Mungu. Kuwa mwanga na chumvi katika kupambana na maovu aina na hasa
mmomonyoko wa maadili. Huu ndiyo wakati wa kuweka na kuingiza roho ya Injili katika
malimwengu. Kuishi maisha yanayoongozwa na tunu za Injili.
MLANGO
WA IMANI: BARUA YA KITUME YA BABA MTAKATIFU BENEDIKTO XVI KUTANGAZA MWAKA WA IMANI.
‘Mlango
wa Imani (Mdo14:27) daima umefunguliwa kwa ajili yetu na kutuongoza katika muungano
na Mungu na kutuingiza ndani ya Kanisa lake. Inawezekana kuvuka kizingiti hicho pale
neno la Mungu linapotangazwa na moyo unapojiruhusu kuundwa kwa kugeuzwa na neema.
Kupita katika mlango huo ni kuanza safari itakayodumu kwa maisha yote.
Safari
hii inaanza na ubatizo (rej. Rum 6:4), ambao kwao tunaweza kumwita Mungu Baba, na
inaisha kwa njia ya kifo kuelekea uzima wa milele, ulio tunda la ufufuko wa Bwana
Yesu, ambaye shabaha yake ilikuwa kuwavuta wale wanaomwamini katika utukufu wake kwa
njia ya Roho Mtakatifu (rej. Yn 17:22). Kukiri imani katika Utatu Mtakatifu: Baba,
Mwana na Roho Mtakatifu ni kuamini katika Mungu mmoja ambaye ni upendo (rej. 1 Yn
4:8): Baba, ambaye katika utimilifu wa wakati alimtuma mwanaye kwa ajili ya wokovu,
wetu Yesu Kristo, ambaye kwa fumbo la kifo chake na ufufuko aliukomboa ulimwengu Roho
Mtakatifu ambaye analiongoza Kanisa katika karne zote tunaposubiri ujio mtukufu wa
Bwana.
Upyaisho wa Kanisa unapatikana pia kwa njia ya ushuhuda
unaotolewa kwa maisha ya waamini; kuishi kwa ulimwenguni, wakristo wanaalikwa kutangaza
neno la ukweli ambalo Bwana Yesu alituachia. Mtaguso wenyewe, katika Konsitusio ya
Kidogma juu ya Fumbo la Kanisa, unasema; Kristo aliye mtakatifu, asiye na uovu asiye
na waa lolote (Ebr 7:26) hakujua dhambi (taz. 2 Kor 5:21) bali alikuja ili afanye
suluhu kwa dhambi za watu (taz. Ebr. 2:17) Kanisa ambalo huwakumbatia wakosefu ndani
yake na wakati ule ule ni takatifu na linahitaji kutakaswa haliachi kamwe kutubu na
kujitengeneza upya.
Kanisa linaendelea mbele katika kuhiji kwake
katikati ya madhulumu ya ulimwengu na faraja za Mungu likitangaza msalaba na mauti
ya Bwana hata ajapo (taz. 1 Kor 11:26). Kwa uwezo wa Bwana aliyefufuka linapata nguvu
ya kuzishinda kwa saburi na upendo, taabu na shida za ndani na za nje, naya kuufunulia
ulimwengu, kwa uaminifu fumbo la Bwana ingawa bado lipo katika kivuli, mpaka mwisho
wa nyakati litakapodhihirishwa katika ukamilifu wa mwanga wake.
Mwaka wa
imani kwa mtazamo huu ni mwaliko wa wongofu wa kweli, uliofanywa upya kwa Bwana, Mwokozi
pekee wa ulimwengu. Katika fumbo la kifo na ufufuko wake, Mungu amefunua katika ukamilifu
wake upendo unaookoa na kutualika sisi kwa wongofu wa maisha kwa njia ya maondoleo
ya dhambi (Mdo 5:31). Kwa Mtakatifu Paulo, Upendo huu unatupeleka kwenye maisha mapya:
‘basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo
alivyofufuka katika wafu kwa nji ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende
katika upya wa uzima’ (Rum 6:4).
Kwa njia ya imani maisha haya mpya yanaunda
uhai wote wa mwanadamu kadiri ya uhalisia mpya usiotetereka wa ufufuko. Kwa kadiri
ile ambayo, kwa uradhi wote mtu anashiriki fumbo hili, mawazo ya mwanadamu na shauku
zake, mtazamo na tabia zake zinaanza kutakaswa na kubadilishwa taratibu, katika safari
ambayo kamwe haikamiliki katika maisha haya. ‘Imani itendayo kazi kwa upendo’ (Gal
5:6) inakuwa ni kigezo kipya cha uelewa na utendaji unaoyabadilisha maisha yote ya
mwanadamu (Rej. 12:2; Kol 3:9-10; Efe 4:20-29;2 Kor5:17).