Ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa ajili ya Siku ya 49 Kuombea Amani Duniani
kwa Mwaka 2013
Heri wapatanishi ndiyo kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya 49 ya Siku ya Kuombea
Amani Duniani kwa Mwaka 2013, sanjari na kumbu kumbu ya miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa
Pili wa Vatican, ulioimarisha utume wa Kanisa ulimwenguni, kwa kutambua kwamba, Familia
ya Mungu inafanya hija ya kihistoria na binadamu wote kwa kushirikishana furaha, matumaini,
machungu na magumu wakati ikiendelea kutangaza Habari Njema ya Wokovu na kutetea amani
kwa wote.
Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe wake wa Siku ya Kuombea Amani Duniani inayokwenda
sanjari na Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu, anabainisha kwamba,
kuna kinzani na migogoro mingi inayoendelea kufuka moshi kutokana na kuongezeka kwa
pengo kati ya maskini na matajiri, binafsi pamoja na athari za mfumo wa ubepari unaokumbatia
mno faida.
Bado kuna vitendo vya kigaidi, makosa ya jinai, misimamo mikali
ya imani inaendelea kuhatarisha amani na asili ya dini ya kweli inayopaswa kimsingi
kukuza na kudumisha udugu na upatanisho kati ya watu. Mwanadamu ana wito unaobubujika
kutoka katika undani wake unaotamani furaha na mafanikio.Mwanadamu anatamani kupata
amani inayoambatana na haki na wajibu na kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi
Mungu. Kauli mbiu ya Mwaka 2013 inapata chimbuko lake katika Heri za Mlimani: Heri
wapatanishi maana wataitwa wana wa Mungu.
Hizi ni heri ambazo watabarikiwa
kuzipata wale wanaojitoa bila ya kujibakiza katika kutafuta ukweli, haki na upendo,
daima wakitambua kwamba, katika mahangaiko yote Mungu yuko pamoja nao na kuwa wakimkubali
Yesu, Mungu kweli na Mtu kweli, wataweza kushiriki maisha ya kimungu, yaani neema
yake, kwani Kristo ndiye anayemkirimia mwanadamu amani ya kweli, akikumbuka kwamba,
amani ni zawadi inayoimarishwa kwa juhudi za kibinadamu, katika mchakato wa kuishi
na kushirikishana na wengine, kama sehemu ya kanuni maadili ambazo kimsingi ni sheria
ya Mungu iliyoandikwa katika moyo wa mwanadamu. Amani inajengwa na kudumishwa kwa
kuzingatia akili na maadili.
Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, amani ni zawadi
kutoka kwa Mwenyezi Mungu na matunda ya kazi ya binadamu inayojionesha kwa kuwa na
utilivu wa ndani, kwa kuishi vyema na jirani pamoja na kujali mazingira. Papa Yohane
wa Ishirini na tatu katika Waraka wake Amani Duniani, Pacem In Terris anakazia mambo
makuu manne ili kuweza kudumisha msingi wa amani: Ukweli, Uhuru, Upendo na Haki.
Hizi
ni tunu msingi zinazomwezesha mwanadamu kuufahamu ukweli, uzuri na uwepo wa Mungu
ambaye ni Muumbaji, kama njia ya kuendelea kuwa ni wapatanishi pamoja na kukuza majadiliano
na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo. Amani inapatikana pale
tu watu wanapotambua kwamba, wao mbele ya Mungu wanaunda Familia Moja ya binadamu
inayoonesha uhusiano, wajibu na majukumu yak ila mtu. Amani inamwilishwa katika upendo
kwa kushirikiana na kufanya kazi na wengine kwa ajili ya mafao ya wengi. Amani ni
jambo linalowezekana na wala si wazo la kufikirika tu! Ndiyo maana Kanisa linaendelea
kumtangaza Yesu Kristo msingi wa maendeleo endelevu na amani ya kweli. Ujenzi wa amani
ni dhamana yak ila mtu!
Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, wapatanishi ni watu
wanaopenda fadhila ya upendo na kuendeleza maisha katika utimilifu wake, kwa kumheshimu
mtu katika hatua zake mbali mbali za ukuaji na kamwe hawezi kukumbatia utamaduni wa
kifo unaojidhihirisha katika sera za utoaji mimba. Ni mtu anayejali maendeleo pamoja
na utunzaji wa mazingira. Ni vyema kuzingatia na kuheshimu kanuni na misingi bora
ya maisha ya ndoa, kwa kutambua na kuthamini utume wake kwa Jamii husika mintarafu
asili ya binadamu. Kanisa linaposimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha
ya ndoa linafanya hivi kwa ajili ya mafao ya wengi, kinyume chake ni kupotosha ukweli,
haki na amani. Watu wajenge dhamiri nyofu ili kusimama kidete kutetea zawadi ya maisha,
ut una heshima ya binadamu dhidi ya vitendo vya utoaji mimba na kifo laini.
Uhuru
wa kuabudu ni sehemu ya haki msingi za binadamu na kigezo muhimu katika kudumisha
misingi ya amani kimataifa. Kuna dalili nyingi za uvunjifu wa misingi ya uhuru wa
kuabudu, unaowazuia watu kutolea ushuhuda wa imani yao, kwa kuiungama na kuimwilisha
hadharani na katika shughuli mbali mbali zinazopania kumletea mwanadamu maendeleo
ya kweli. Sehemu mbali mbali za dunia, Wakristo wanaendelea kudhulumiwa.
Wapatanishi
hawana budi kutambua kwamba, shinikizo linalotolewa katika maoni, sera na uhuru usiokuwa
na mipaka lazima yajikite katika uwajibikaji, mshikamano, haki na wajibu. Kazi ni
wajibu wa kijamii unaopaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa kwa kupewa ujira unaostahili
badala ya mfumo wa sasa kazi kuongozwa na mfumo wa uchumi huria na hivyo kupimwa kwa
vigezo vya fedha na uchumi.
Kuna haja ya kuendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha
kwamba, watu wengi zaidi wanapata fursa ya kazi kwa kuzinatia misingi ya maadili na
tunu bora za maisha ya kiroho, kwa kutambua kuwa kazi ni kwa ajili ya mafao ya mtu
binafsi, familia na Jamii katika ujumla wake. Kutokana na mwelekeo huu kuna haja ya
kuwa na sera makini za fursa za ajira.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita, anahamasisha ujenzi wa amani ya kweli kwa njia ya miundo bora ya maendeleo na
uchumi inayojikita katika mshikamano na mafao ya wengi kwa kutambua pia uwepo wa Mungu
ili kupata maisha bora zaidi. Ili kuondokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa,
kuna haja kuwa na ugunduzi utakaobainisha mifumo mipya ya uchumi dhidi ya watu kutafuta
faida kubwa inayogubikwa na ubinafsi na ulaji wa kupindukia. Watu wajitoe sadaka kwa
kutumia vyema karama na mapaji waliyokirimiwa na Mwenyezi Mungu katika maisha yao,
ili yatumike kwa ajili ya mafao ya wengi, huku wakizingatia udugu; usawa na hali ya
kutegemeana, daima wakilenga mafao ya wengi, kwa sasa na kwa kizazi kijacho.
Maendeleo
ya uchumi, uzalishaji viwandani na katika sekta ya kilimo, yanahitaji kwa namna ya
pekee kabisa uwepo wa misingi ya kimaadili kuhusu biashara na soko la fedha; uhakika
na usalama wa chakula na mfumuko wa bei ya chakula; hali ambayo ni tete zaidi kuliko
hata athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Wapatanishi wajenge na kudumisha mshikamano
katika ngazi mbali mbali, hasa kwa kuwasaidia wakulima wadogo wadogo vijijini kutekeleza
wajibu wao katika mazingira bora zaidi, wakilinda na kutunza mazingira sanjari na
maboresho ya uchumi.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe
wake kwa Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2013 anagusia umuhimu wa elimu kama
sehemu ya ujenzi wa utamaduni wa amani kwa kuiangalia familia pamoja na taasisi mbali
mbali zinazopaswa kujikita katika kutafuta mafao ya familia na haki jamii bila kusahau
umuhimu wa kuwa na elimu jamii makini. Familia ipewe kipaumbele cha kwanza katika
majiundo ya mtu kwenye medani mbali mbali za maisha na kwamba, familia inawajibu wa
kulinda na kutetea maisha, kulea, kutunza na kushirikishana.
Hapa ni mahali
pa kujenga na kukuza utamaduni wa amani; kwa kutambua kuwa wazazi wanawajibu na dhamana
ya kutoa elimu kwa watoto wao kimaadili na kiroho. Watoto warithishwe utamaduni wa
kupenda na kuthamini zawadi ya maisha. Jumuiya za kidini zitekeleze pia wajibu wake
kama sehemu ya mchakato wa Unjilishaji Mpya; daima wakijitahidi kufanya toba na wongofu
wa ndani; kwa kujikita katika maisha ya kiroho na adili sanjari na kusimama kidete
kupinga ukosefu wa haki.
Taasisi za elimu, shule na vyuo vikuu vina dhamana
ya kudumisha amani, kwa kutoa malezi ya viongozi wa leo na kesho pamoja na kuleta
mabadiliko muhimu katika taasisi za kiserikali kitaifa na kimataifa. Wafanye tafiti
za ufumbuzi wa matatizo ya kiuchumi na kifedha kwa kuzingatia ut una tunu msingi za
kimaadili. Wanasiasa wajitahidi kutafuta kwanza kabisa mafao ya wengi pamoja na kukuza
ushirikiano na mshikamano kwa ajili ya ukuaji wa mtu binafsi na makundi kama msingi
wa kweli wa elimu ya amani.
Baba Mtakatifu anaendelea kuhamasisha umuhimu wa
kufundisha utamaduni wa amani kwa ajili ya mafao ya wengi, kwa njia ya mawazo, maneno,
matendo na kwa kutimiza wajibu. Watu wajifunze kupendana, kuthaminiana na kuvumiliana.
Wakatae tabia ya kulipiza kisasi na badala yake wakumbatie fadhila ya kusamehe wakipania
kujenga msingi wa msamaha na upatanisho wa kweli. Amani ya kweli inajidhihirisha katika
matendo, huruma, mshikamano, ujasiri na udumifu, kama anavyobainisha Yesu Kristo mwenyewe
kwa njia ya maisha yake.
Ni mwaliko kwa kila mwamini kumwomba Mungu amwezeshe
kuwa ni mjenzi wa amani; viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa wajibidishe katika kutafuta
amani kwa kubomoa kuta zinazowatengenanisha na kuimarisha kifungo cha upendo, uelewano,
msamaha na udugu ili kweli amani iweze kutawala na kudumu.