Maamuzi ya Baraza la Madaktari kuhusu madaktari waliogoma nchini Tanzania
Kutokana na mgomo wa madaktari uliotokea kati ya tarehe 23 na 29 mwezi Juni 2012.Wizara
iliwasilisha malalamiko kwenye Baraza la Madaktari Tanganyika ili lifanye uchunguzi
kuhusu madaktari hao.
Idadi ya madaktari wote waliogoma walikuwa 394, kati
yao madaktari 376 walikuwa ni madaktari walio katika mafunzo kwa vitendo (Interns)
kutoka hospitali za Muhimbili, K.C.M.C. Bugando, Mbeya Rufaa, St. Francis - Ifakara,
Dodoma, Temeke, Mwananyamala, Amana, Haydom na Sekou Toure. Aidha, Madaktari waajiriwa
(Registrar) 18 walishiriki katika mgomo huo kutoka hospitali ya Rufaa ya Mbeya.
Baraza
lilipitia malalamiko yote na limetoa adhabu stahiki kwa kila daktari aliyethibitishwa
kushiriki katika mgomo huo. Adhabu hizo zilikuwa katika makundi yafuatayo; onyo,
onyo kali na kusimamishwa udaktari kwa muda wa kati ya mwezi mmoja na miezi sita.Vile
vile kuna Madaktari ambao hawakuwa na hatia ya kushiriki katika mgomo na hivyo walifutiwa
mashtaka.
MCHANGANUO WA ADHABU ·Waliofutiwa mashitaka madaktari 49 ·Waliopewa
onyo madaktari 223 ·Waliopewa onyo kali madaktari 66 ·Kusimamishwa kwa muda
madaktari 30 ·Mashitaka yaliyoahirishwa kutokana na wahusika kuhitaji ushauri wa
kisheria madaktari 4 ·Mashitaka yasiyosikilizwa kutokana na wahusika kutofika walipoitwa
na Baraza madaktari 22
Wizara inakamilisha taratibu za kinidhamu kwa mujibu
wa Kanuni za Utumishi wa Umma kwa Madaktari wote waajiriwa ambao walipatikana na hatia
mbele ya Baraza la Madaktari. Wizara pia imeridhia kuwapa Madaktari waliokuwa katika
mafunzo kwa vitendo fursa nyingine ya kuendelea na mafunzo hayo katika hospitali za
Umma walizokuwepo kabla ya kuondolewa. Hata hivyo fursa hii haitawahusu Madaktari
wote waliopewa adhabu za kusimamishwa na Baraza la Madaktari, hadi hapo watakapomaliza
kutumikia adhabu zao.
HITIMISHO
Kwa taarifa hii madaktari wote waliofutiwa
mashtaka na wale waliopewa onyo na onyo kali wanatakiwa kuwasilisha kwa Katibu Mkuu
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii barua kutoka kwa msajili wa Baraza la Madaktari
ikithibitisha kurejeshewa usajili na kuruhusiwa kuendelea na mafunzo kwa vitendo.
Vile vile madaktari waajiriwa (Registrar) wanatakiwa pia kuripoti kwa Katibu Mkuu
Wizara ya Afya ili kupewa barua zao kulingana na Adhabu walizopewa.
Barua
hizi zitatolewa kuanzia tarehe 2 Januari, 2013. Madaktari wote walio katika mafunzo
kwa vitendo wanatakiwa kuanza kazi katika vituo vyao vya awali ifikapo tarehe 14
Januari, 2013.Hakuna muda utakaoongezwa kwa kipindi kilichobakia cha mafunzo kwa vitendo.
Kwa wale wote waliopewa adhabu wataanza kutumikia adhabu hizo kuanzia tarehe ya adhabu
hiyo ilivyotolewa.