2012-12-27 09:27:30

Kanisa linamwimbia Mungu utenzi wa shukrani kwa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican


Mama Kanisa anaendelea kumshukuru Mungu kwa wema na ukarimu ambao amelijalia katika kipindi cha Mwaka 2012. Ni mwaka ambao umefumbata hija ya maisha ya kiimani inayomshirikisha mwamini maisha na utume wa Yesu Kristo, aliyezaliwa, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Huu ndio msingi wa maadhimisho ya Mwaka wa Kanisa.

Ni sehemu ya ujumbe wa Mheshimiwa Padre Dietrich Pendawazima, Makamu Mkuu wa Shirika la Waconsolata Ulimwenguni, wakati akitoa salam na matashi mema kwa Familia ya Mungu popote pale ilipo wakati huu wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli na Mwaka Mpya 2013.

Anasema, kuzaliwa kwa Yesu Kristo kati ya watu wake, yaani Emmanuel, kunaonesha: imani na matumaini ya watu wenye mapenzi mema, ambao wako tayari kumkaribisha Mwenyezi Mungu ili aweze kuzaliwa tena katika maisha na vipaumbele vyao vya maisha. Ni changamoto endelevu kwa waamini kumuungama, kumtangaza na kumshuhudia Kristo katika uhalisia wa maisha yao, kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.

Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican anasema Padre Pendawazima ni kati ya zawadi kubwa ambazo Mwenyezi Mungu kwa njia ya Yesu Kristo amelizawadia Kanisa. Ni Mtaguso ambao umekuwa ni dira na mwongozo kwa maisha na utume wa Kanisa katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Ni Mtaguso ambao umetoa msukumo wa pekee katika kumfahamu Mungu aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo; Neno wa Mungu aliyefanyika Mwili.

Mtaguso wa Pili wa Vatican una utajiri mkubwa ambao unapania kuwajengea uwezo waamini kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu unaosimikwa katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano; kwa kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini na kiekumene; kwa pamoja wakitafuta mafao ya wengi; kwa kuheshimu na kuthamini utu wa mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Waamini wanahamasishwa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kumwilisha Neno la Mungu na Liturujia katika uhalisia wa maisha yao, kama njia ya kuyatakatifuza malimwengu sanjari na kuendeleza kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe.

Padre Dietrich Pendawazima anasema, changamoto zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, uwawezeshe waamini kusoma alama za nyakati, tayari kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa bila hata ya kujibakiza.







All the contents on this site are copyrighted ©.