2012-12-26 09:39:31

Watanzania kamwe msikubali kukumbatia utamaduni wa kifo! Dumisheni misingi ya haki, amani na upendo!


Askofu mstaafu Mathias Joseph Issuja wa Jimbo Katoliki Dodoma anawataka watanzania kupinga kwa nguvu zao zote sera za utoaji mimba pamoja na udhibiti wa ongezeko la watu, kwani vitendo hivi ni kikyume kabisa cha mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wake.

Askofu Issuja ameyasema hayo wakati wa mahubiri katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba. Anawahimiza watanzania wakati huu wanapoendelea kuchangia maoni yao kwenye Tume ya Kukusanya Maoni ya Katiba Mpya, kupinga ser na mikakati inayopania kukumbatia utamaduni wa kifo.

Askofu Issuja amekazia kwa namna ya pekee, umuhimu wa watanzania kuendelea kulinda, kutunza na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa, ili kuendeleza mafanikio yaliyokwisha kupatikana nchini Tanzania kwa takribani miaka hamsini na moja iliyopita. Bila misingi ya haki, amani na usawa, taifa linaweza kujikuta likitumbukia katika maafa. Amani si bidhaa inayoweza kuuzwa au kununuliwa sokoni, bali ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayowajibisha pia binadamu.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia yasaidie pia maboresho na uelewa wa watu wengi kuhusu hali yao ya maisha pamoja na kupambana na hali mbali mbali kisayansi badala ya kuendekeza mila na desturi zilizopitwa na wakati. Maendeleo na mafanikio yanapatikana kwa kufanya kazi kwa: bidii, juhudi na maarifa na wala hakuna njia ya mkato kwa kukimbilia kwa waganga, matokeo yake ni mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, hali inayojenga hofu na wasi wasi miongoni mwa Jamii. Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yaimarishe imani, matumaini na mapendo katika Jamii kama njia ya ushuhuda wa Imani katika matendo.







All the contents on this site are copyrighted ©.