2012-12-26 08:28:27

Ukweli na uwazi ni muhimu katika matumizi ya rasilimali ya Kanisa


Idara ya uchumi, fedha na mipango ya Vatican inapania kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, shughuli zinazoendeshwa na Vatican katika masuala ya uchumi na fedha, zinazingatia misingi ya ukweli na uwazi, kama ilivyobainishwa kwenye Taratibu Mpya zilizopitishwa tarehe 22 Februari 2012 na kuanza kutumika hivi karibuni. RealAudioMP3

Hayo yamebainishwa na Kardinali Giuseppe Versaldi pamoja na viongozi wengine waandamizi kutoka katika Idara hiyo walipokuwa wanaelezea utekelezaji wa kanuni hizi ambazo kwa sasa zina mwelekeo wa kimataifa. Ukweli na uwazi katika masuala ya fedha na uchumi ni mambo muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa; ndani na nje ya Kanisa lenyewe. Mchakato huu unapania pamoja na mambo mengine, kuimarisha uaminifu kwa Kanisa na utume wake ulimwenguni.

Idara ya uchumi, fedha na mipango ya Vatican inasimamia, kuratibu na kudhibiti shughuli zote za uchumi, fedha na mipango zinazoendeshwa mjini Vatican; mintarafu misingi ya ukweli na uwazi. Licha ya kuwaamini watu wanaotekeleza wajibu na majukumu yao katika masuala haya, lakini, hiki ni chambo cha juu kabisa cha kusimamia fedha na mali ya Vatican.

Katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia pamoja na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, Kanisa limejifunza kwa namna ya pekee kuhakikisha kuwa linatumia vyema mchango unaotolewa na wafadhili mbali mbali kwa ajili ya kulitegemeza Kanisa katika maisha na utume wake ulimwenguni, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wahitaji zaidi.

Idara ya uchumi, fedha na mipango pamoja na mambo mengine itakuwa na dhamana ya kuratibu na kudhibiti shughuli zote za uchumi na fedha zinazofanywa na Vatican pamoja na vitengo vyake vyote, kama alivyokuwa amebainisha Papa Paulo wa sita, kunako tarehe 15 Agosti 1967 alipokuwa anaanzisha Idara hii. Kwa sasa Idara hii pia itajishughulisha na kupanga na kuelekeza shughuli mbali mbali zinazofanywa na Vatican.

Askofu mkuu Vallejo Balda; katibu mkuu wa Idra ya uchumi, fedha na mipango anasema, kwamba, makucha ya athari za myumbo wa uchumi kimataifa yameanza kugusa hata uchumi wa Vatican. Kwa miaka kadhaa kwa sasa, mapato na matumizi ya Vatican yamekuwa hayalingani, kwani kuna matumizi makubwa zaidi kuliko mapato ya Kanisa. Mchango unaotolewa na Waamini pamoja na wafadhili mbali mbali haukidhi gharama za uendeshaji wa shughuli na mikakati mbali mbali ya Vatican.

Sehemu kubwa ya mapato ya Vatican yanaelekezwa zaidi kwenye mishahara ya wafanyakazi wake ambao kwa sasa wamefikia elfu tano na mia tano. Ni fedha inayotumika kulipa pensheni na huduma za tiba.

Licha ya mikakati mbali mbali inayotolewa ili kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za Vatican ili kuliwezesha Kanisa kuendelea kutoa huduma yake sehemu mbali mbali za dunia; Vatican inapania kuhakikisha kwamba, rasilimali fedha na vitu vilivyopo vinatumika barabara, na hasa zaidi kwa ajili ya kuwasaidia maskini na wahitaji zaidi, jambo ambalo pengine halifahamiki na wengi au halijapewa uzito wa kutosha.








All the contents on this site are copyrighted ©.