Jitokezeni kushiriki katika chanjo ya kuzuia kichomi kwa watoto!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda, amewataka Watanzania wote kushiriki chanjo
ya kuzuia kichomi na kuhara kwa watoto pindi itakapoanza kutolewa mapema mwakani.
Ametoa wito huo Jumanne, Desemba 25, 2012 wakati akizungumza na maelfu ya wakazi wa
kata ya Kibaoni na kata jirani za Ikuba, Usevya, Mbede, Mamba na Majimoto walioshiriki
kula naye chakula cha mchana kuadhimisha Sikukuu ya Noeli.
Sherehe hizo zilifanyika
kwenye uwanja wa shule ya msingi Kakuni ambako pia ni kijijini kwake kata ya Kibaoni,
wilayani Mlele, mkoani Katavi. “Serikali itaanza kutoa chanjo ya kuzuia kichomi (kitaalam
wanaiita pneumonia) na ya kuzuia kuhara. Magonjwa haya mawili yana madhara makubwa
kwa watoto wadogo. Natoa wito kwa Watanzania wake kwa waume, wakati ukifika wapelekeni
watoto kwenye hiyo chanjo ili kuokoa maisha yao,” alisisitiza.
Alitumia fursa
hiyo kuwahimiza wakazi wa kata hizo kununua vyandarua na kuvitumia ili kujikinga na
ugonjwa wa malaria kwa vile ndiyo unaoongoza kwa vifo nchini kuliko magonjwa mengine.
“Nawasihi wafugaji, ninyi mna hela… uzeni mifugo ili mpate fedha ya kununua chandarua,
takwimu zinaonyesha kuwa kila baada ya dakika tano kuna mgonjwa anakufa kutokana na
malaria. Kwa hiyo mtu akipata visenti vyake, anunue chandarua kwa mkewe na watoto,”
alisisitiza.
Akizungumzia kuhusu UKIMWI, Waziri Mkuu alitaka wakazi wa Jimbo
lake la Katavi kutambua kwamba ugonjwa huo upo na kwamba hauna tiba na tena hauchagui
kijana wala mzee, kijana wa kiume au wa kike. “Ninachowasisitiza hapa ni kwamba mtambue
kuwa kuwa ugonjwa huu upo tena hauna tiba. Kilichopo sasa ni dawa za kupunguza makali
ya virusi ambazo zinasaidia kurefusha maisha. Ugonjwa huu hauchagui kijana wala mzee,
hauchagui kijana wa kiume wala wa kike. Ni lazima tujihadhari,” alisisitiza.
Hivyo,
aliwasihi waende kupima kwa hiari kwenye hospitali ya wilaya au wakati wa maonyesho
ili waweze kujitambua hali zao na kufuata ushauri watakaopewa baada ya kupokea matokeo.
“Kama umeambukizwa utapewa ushauri wa namna ya kuishi, ukikutwa hujaambukizwa pia
utaelezwa namna ya kuchukua tahadhari ili usipate maambukizi mapya,” alisema.
Kuhusu
kilimo na ufugaji nyuki, Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwasihi wakazi wa kata hizo
wafanye kazi kwa bidii na maarifa ili waweze kupata mabadiliko ya haraka katika kujiletea
maendeleo yao kiuchumi.