2012-12-25 11:39:29

Kanuni ya Imani ni muhtsari wa Imani, dira na mwongozo katika hija ya maisha ya waamini hapa ulimwenguni


Waamini wanatakiwa kuwa watenda haki, wavumilivu, wastahimilivu na kuepuka kutumia njia za mabavu na vitisho katika masuala mbalimbali ya kimaisha na kwamba hiyo ndiyo neema pekee ya utashi itakayowafikisha mbinguni pamoja na kuendelea kuifanya dunia kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Waamini wajikite katika maisha ya sala, tafakari ya kina ya Neno la Mungu, matendo ya huruma, kama njia makini ya ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, wakati huu, dunia inaposhangilia kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa ulimwengu.

Hayo yamesemwa na Askofu Evaristo Chengula (IMC) wa Jimbo Katoliki Mbeya wakati wa maadhimisho ya ibada ya misa takatifu ya mkesha wa siku kuu ya noeli; kuzaliwa kwake Yesu Kristo iliyofanyika katika Kanisa kuu la Mtakatifu Anthony wa Padua Parokia ya Mbeya Mjini Kuzaliwa kwake Yesu Kristo Mwana wa Mungu; wakristo Wanapaswa kuutumia fursa ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kutafakari tabia, kuthibitisha na kukiri imani na matumaini yaliyopandikizwa katika mioyo ya waamini.

Aliwakumbusha kuwa Kanuni ya Imani inawataka Wakristo kusadiki kwa Mungu mmoja hata kama mambo yanayojitokeza ni magumu na makubwa kuliko maumbile ya mwanadamu huku unyenyekevu upole, haki na amani vikitawala. "Kristo alifauru katika ukombozi wake wa dunia kwa sababu hakutumia mabavu katika maamuzi yake hadi walimuuwa kwa hiyo imani yetu inakwenda kwa njia ya unyenyekevu, lakini kwa neema ya Mwenye Mungu tunaweza kufauru katika kila jambo,"alisema.

Askofu Chengula alisema, mara nyingi Kanisa lina mwono wa nguvu nguvu jambo ambalo Yesu Kristo anawakumbusha kwamba, wanapaswa kuwa wanyenyekevu katika masuala mbalimbali hivyo, kujiunga na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika kutolea ushuhuda wa Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Imani. "Wengi wanajifunza na kusoma Biblia na Taalimungu lakini siyo wote wanaweza wakawa na imani siyo sababu ya kusoma sana, bali ni neema na zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kanuni ya imani iwe ni kioo cha imani ya Kikristo, lazima tujiangalie sisi wenyewe kama kweli tunasadiki na kufurahia imani hii kila siku na itawafanya wenye heri katika uzima ujao,"alisema.

Alisema bila kuwa wenzi wa Roho Mtakatifu waimbaji hawataweza kuwashirikisha waamini kiasi hata cha kuguswa na nyimbo zao licha ya kufanya kazi ya kitume kwani bila kuuwisha na Roho Mtakatifu yote ni bure na mwisho wasio kuwa na Roho mtakatifu watabakia pembeni kuwapisha wenye imani. Hata waumini wanaopanda mbele ya Altar kama hawana ndani mwao Rho Mtakatifu masomo yao yataingia katika sikio la kulia na kutokea la kushoto, hayaingii akilini mwake na kwa waumini na hivyo kuwa sawa na bure.

Askofu Chengula alisema mwaka 2013 Jimbo Katoliki la Mbeya litafungua mchakato wa Sinodi ya Jimbo ambapo kila mwamini atapaswa kutafakari baada ya programu kutolewa Januari,10,2013 katika siku ya kuadhimisha Jubilee ya miaka 25 ya baadhi ya Mapadre Jimboni na baadaye itafuatia utekelezaji wa maamuzi yaliyotolewa na Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika, mintarafu vipaumbele vya Jimbo Katoliki Mbeya, Kanisa la Tanzania na Afrika katika ujumla wake.

Katika Ibada ya Misa Takatifu, Askofu Chengula amebariki na kuzindua Kinanda kipya kikubwa na ngoma kwa ajili ya kwaya ambavyo vimenunuliwa kwa misaada ya waumini mbalimbali waliojitolea na amewashukuru waumini kuendelea kujitoa kulichangia kanisa katika masuala mbalimbali na huo ndiyo utume.









All the contents on this site are copyrighted ©.