2012-12-22 09:37:40

Msimamo wa Kanisa kuhusu adhabu ya kifo unafafanuliwa vyema kwenye Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican amekanusha taarifa zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba, viongozi kadhaa wa Serikali ya Uganda wanaotembelea Roma, walipokutana na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, mara baada ya Katekesi yake siku ya Jumatano, tarehe 19 Desemba 2012 walipata baraka kwamba anaunga mkono adhabu ya kifo kwa wale watakaopatikana na hatia ya kujihusisha na ndoa za watu wa jinsia moja, jambo ambalo si kweli kabisa!

Padre Lombardi anasema, uvumi huu unakwenda kinyume kabisa na mafundisho ya Kanisa na msimamo wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuhusu adhabu ya Kifo. Kusalimiana na mtu si tiketi ya kuhalalisha sera za nchi husika. Rebeka Kadaga ni kati ya viongozi wa ngazi za juu kutoka Uganda waliohudhuria Katekesi ya Baba Mtakatifu, Jumatano iliyopita na kwamba, binafsi anaunga mkono adhabu ya kifo dhidi ya watu watakaopatikana na hatia hiyo.

Padre Lombardi anabainisha kwamba, mafundisho ya Kanisa kuhusu adhabu ya Kifo yanafafanuliwa kwa kina na mapana na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Muswada wa sheria dhidi ndoa za watu wa jinsia moja unaendelea kupingwa na watu mbali mbali ndani na nje ya Uganda.







All the contents on this site are copyrighted ©.