2012-12-21 07:25:03

Ujumbe wa Noeli: tunataka viongozi wadhihirishe kwa vitendo: uadilifu, uaminifu, ukweli, uzalendo na uchungu kwa nchi yao!


Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina wakati huu wa Kipindi cha Noeli, linasema katika tafakari yake kwamba, wananchi wa Argentina wanahamu ya kusikia na kuonja kuwa, viongozi nchini humo wanadhamiria kuonesha dira ya maendeleo endelevu kwa kudhihirisha kwa matendo: uadilifu, uaminifu, ukweli, uzalendo na uchungu kwa nchi yao. RealAudioMP3

Viongozi wanaojifikiria na kujitafuta wenyewe na kwa mafao yao binafsi hawana tena nafasi ya kupewa dhamana ya kuiongoza nchi. Viongozi watafute kwanza kabisa mafao ya wengi.

Hii ni tafakari ya kina iliyofikiwa na Maaskofu Katoliki Argentina mara baada ya mkutano wa mia moja nan ne, uliojadili pamoja na mambo mengine Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliozinduliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Maaskofu katika ujumbe wao, wanapenda kuwaelekezea zaidi viongozi ncghini Argentina kwamba, wanayo dhamana kubwa nan yeti inayowakumbusha kwamba, watu bado wana imani kwamba, wanaweza kujifunga kibwebwe kujenga nchi katika moyo wa udugu na mshikamano wa kitaifa.

Maaskofu wanafanya upembuzi wa kina kuhusu hali halisi ya maisha ya wananchi wa Argentina ambao wanakabiliana na mmong’onyoko wa maadili na utu wema; mambo ambayo yanagusa hata misingi ya kitamaduni. Sheria za nchi hazina budi kuwalinda wanyonge badala ya kukumbatia utamaduni wa kifo na athari zake zinazojionesha katika tunu bora za maisha ya kifamilia. Kuna mwelekeo wa kutaka kutunga sheria zinazosigana na utu pamoja na heshima ya binadamu.

Mfumo wa elimu hauna budi kutoa nafasi kwa wazazi na walezi kuamua kuhusu hatima ya watoto wao kwa siku za usoni, kwani wanatambua dhamana na utume wao katika mchakato mzima wa malezi na makuzi ya watoto ndani ya Jamii. Kuna kundi kubwa la vijana wa kizazi kipya linaonekana kukata tamaa na kukosa dira na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi. Ni kundi ambalo wengi wao hawana hata nafasi ya kuendelea na masomo, kwani kimsingi elimu ni ufunguo wa maisha.

Maaskofu wanasema kwamba, kuna ongezeko kubwa la mtandao wa biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya, hali ambayo inapelekea ongezeko la vitendo vya jinai pamoja na ukosefu wa amani, usalama na utulivu kwa wananchi wengi wa Argentina. Baada ya watu wengi kufurahia matunda ya demokrasia kwa takribani kipindi cha miaka thelathini, kuna hatari kwamba, misingi ya demokrasia ikabomolewa na hivyo kuweka vikwazo kwa watu wengi kushiriki katika masuala ya kisiasa nchini humo.

Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, Maaskofu wanasema, Argentina inataka kuunda jukwaa la majadiliano, mahali pa kukutana na kujenga umoja na udugu; watu wakiwa na dhamiri nyofu ya kutaka kuondokana na sera kandamizi, ubaguzi, chuki na uhasama unaojengwa mioyoni mwa watu kwa mafao ya watu wachache ambao wamefilisika kisiasa.

Nchi alimozaliwa mtu ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na watu wanakabidhiwa kuiendeleza katika uhuru kamili. Licha ya matatizo, vikwazo na changamoto mbali mbali wanazokabiliana nazo wananchi wa Argentina, lakini bado kuna utashi mkubwa wa kutaka kujenga na kuimarisha umoja, udugu na mshikamano wa kitaifa. Kila mtu akitekeleza wajibu wake, kwa hakika jambo hili linaweza kufanikiwa wanasema Maaskofu Katoliki wa Argentina.








All the contents on this site are copyrighted ©.