Salam za Noeli kwa Mwaka 2012 kutoka kwa Patriaki Fouad Twal
Patriak Fouad Twal wa Yerusalem katika ujumbe wake wa Noeli kwa Mwaka 2012; Mwaka
wa Imani sanjari na Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa
Vatican anayaangalia matukio mbali mbali yaliyojitokeza katika kipindi cha Mwaka 2012;
mwaka ambao umekuwa ni chemchemi ya baraka, lakini pia kumekuwepo na machungu ambayo
yamejitokeza katika hija ya maisha ya watu huko Mashariki ya Kati.
Kanisa
limeendelea kudumisha majadiliano ya kiekumene na waamini wa madhehebu mbali mbali
ya Kikristo kwa kuwataka kuendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya nchi zao
kwa kujikita zaidi na zaidi katika misingi ya haki, amani, ukweli, upatanisho na msamaha.
Juhudi hizi zinakwenda sanjari na majadiliano ya kidini na waamini wa dini
ya Kiislam na Kiyahudi; viongozi wa kidini wanakumbushwa kwamba, wana dhana ya kusimama
kidete kulinda na kutetea misingi ya amani na utulivu; kwa kuheshimiana na kuthaminiana
pamoja na kuondoa mbegu ya chuki na uhasama kutoka katika mioyo ya vijana, juhudi
ambazo zinapaswa kuanzia shuleni.
Kwa mara ya kwanza, hapo tarehe 5 Mei 2013
Makanisa ya Mashariki yataanza kuadhimisha kwa pamoja Siku kuu ya Pasaka, isipokuwa
kwa Yerusalem na Bethlehemu mabadiliko haya yataanza kufanya kazi mwaka 2014. Waamini
wa madhehebu na dini mbali mbali walihudhuria wakati wa kusimikwa kwa Papa Tawadros
wa Pili mjini Cairo, kama kielelezo cha kuendeleza majadiliano ya kiekumene ili kujenga
na kuimarisha umoja miongoni mwa Wakristo.
Patriaki Twal anasema, hali ya ulinzi
na usalama huko Mashariki ya Kati bado ni tete, kiasi kwamba, inaweka wingu kubwa
katika maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli kwa mwaka 2012. Kanisa linaendelea kuonesha
mshikamano wake wa dhati kwa kuwapokea na kuwasaidia wakimbizi zaidi 250, 000 waliokimbia
kutoka Syria na kwenda Yordani.
Azimio la Umoja wa Mataifa kuifanya Palestina
kuwa ni kati ya nchi watazamaji wa kudumu wa Umoja wa Mataifa ni hatua ya kuridhisha
katika mchakato wa kutafuta na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu. Ni matumaini
ya viongozi wa Kanisa kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itasaidia kuunda uwepo wa mataifa
mawili yanayojitegemea. Kuna watu zaidi ya millioni moja na nusu wanaoishi katika
Ukanda wa Ghaza, hali waliyo nayo inaonesha kwamba, bado wana chuki na hasira dhidi
ya Israeli.
Kanisa bado linaendelea kuwasaidia wakimbizi ili kupata mahitaji
yao msingi pamoja na kuhakikisha kwamba, sauti yao inasikika katika Jumuiya ya Kimataifa,
hasa pale wanapokabiliana na mashambulizi yasiokuwa na msingi kama ilivyojitokeza
hivi karibuni. Sekta ya elimu ni kati ya njia ambazo Kanisa linaendelea kutumia kama
kielelezo cha majadiliano ya kidini na kiekumene; amani na utulivu miongoni mwa Jamii.
Patriaki
Twal anawahimiza waamini Mashariki ya Kati kuendelea kujitajirisha kwa ujumbe wa Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuhusu Kanisa Mashariki ya Kati, kama njia muafaka
ya kuadhimisha Mwaka wa Imani. Mwishoni mwa mwezi Aprili 2013 kutafanyika mkutano
wa kimataifa mjini Yerusalemu kuhusu maisha ya Papa Yohane wa Ishirini na tatu, muasisi
wa Waraka wa Kichungaji kuhusu majadiliano ya kidini, Nostra Aetate; mkutano ambao
unatarajiwa kuwashirikisha wasomi wa dini ya Kiyahudi.
Vijana kutoka Mashariki
ya Kati wanatarajia pia kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa
Mwaka 2013, huko Rio de Janeiro. Kipindi cha Noeli ni wakati muafaka wa kushirikishana
na kumegeana furaha na shukrani kwa Mwenyezi Mungu na Watu wote wa Mungu popote pale
walipo!