2012-12-21 10:36:25

Ninawaleteeni Habari Njema ya Wokovu: Uinjilishaji Mpya unaojikita katika chemchemi ya furaha!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita pamoja na wasaidizi wake wa karibu, Ijumaa tarehe 21 Desemba 2012 alishiriki katika tafakari ya tatu iliyoandaliwa na Padre Raniero Cantalamessa, O.F.M.Cap. mhubiri wa nyumba ya Kipapa kama sehemu ya maandalizi ya Siku kuu ya Noeli, kwa kujikita zaidi katika tema juu ya Uinjilishaji kielelezo cha furaha ya ndani ya kukutana na Yesu Kristo, kama inavyojionesha pia katika Simulizi za kuzaliwa Mtoto Yesu.

Hii ndiyo furaha ambayo Mzee Zakaria, Elizabeti, Bikira Maria na wachungaji waliokuwa kondeni wakichunga mifugo yao waliionja kwa kusikia Habari Njema ya kuzaliwa kwa Mkombozi wa dunia. Chemchemi ya furaha hii ni kutokana na ukweli kwamba, Mwenyezi Mungu amewakumbuka na kuwatembelea watu wake, tayari kutekeleza ahadi zake kwa wakati muafaka.

Padre Cantalamessa anasema kwamba, kuna haja kwa waamini, baada ya kusikiliza Neno la Mungu kwa umakini katika Liturujia, kuendelea kulimwilisha katika uhalisia wa maisha, kwa kushirikishana furaha hii kubwa ya kuzaliwa kwa Mkombozi wa dunia, kwani hili ni tukio la kihistoria linaloacha chapa ya kudumu katika maisha ya binadamu, kwa kutambua kuwa, Fumbo la Utatu Mtakatifu ndiyo chemchemi ya furaha ya kweli.

Ni furaha inayoashilia mwanzo wa utekelezaji wa kazi ya ukombozi, kama anavyobainisha Bikira Maria katika utenzi wake wa furaha kwa Mwenyezi Mungu, ambaye aliuangalia unyonge wa mjakazi wake; wimbo ambao Mama Kanisa anaendelea kuuimba kwa kumshukuru Mungu kwa matendo yake makuu aliyolikirimia Kanisa katika Kipindi cha Karne ishirini zilizopita.

Mbegu ya ufalme wa Mungu inaendelea kukua na kuchanua kutokana na neema na baraka mbali mbali zinazojionesha ndani ya Kanisa: kuna umati mkubwa wa watakatifu, mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kitume na kwamba licha ya mapungufu na ubinadamu unaojionesha ndani ya Kanisa, lakini nguvu za mauti zimeshindwa kuliangamiza Kanisa la Kristo, kwa hakika hiki ni kielelezo cha uwepo endelevu na utendaji wa Mungu ndani ya Kanisa.

Furaha ya kweli iwe ni mchakato wa toba na wongofu wa ndani, kwa kutambua na kukiri mapungufu yaliyojionesha miongoni mwa Watoto wa Kanisa, tayari kuomba msamaha na kuanza hija inayoelekea kwenye Utakatifu wa Maisha. Waamini wajikite katika tafakari ya kina ya Neno la Mungu, wajitoe kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao; wakionesha mshikamano wa huruma na upendo kwa wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kanisa lijitahidi kujenga na kuimarisha umoja na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Licha ya furaha, lakini mwanadamu anaendelea kukumbana na mazingira yanayoashilia huzuni na mahangaiko, kiasi cha kudhani kwamba, hakuna Mungu, hali inayopelekea watu wengi kukengeuka na kutopea katika malimwengu; matumizi haramu ya dawa za kulevya, mauaji ya kutisha yanayoendelea kutawala katika vyombo vya habari, mmong'onyoko wa maadili na utu wema; ni kati ya mambo ambayo yanamvunja moyo mwanadamu wa leo.

Lakini, waamini wasisahau kwamba, licha ya furaha kubwa iliyoletwa na Habari Njema ya Wokovu, kilele chake ni Fumbo la Msalaba; yaani mateso, kifo na ufufuko wake! Ushindi wa kishindo kuelekea maisha ya uzima wa milele. Mwenyezi Mungu ni mwanga unaoyaangazia mapito ya mwanadamu usiku na mchana; matumaini ambayo kamwe hayawezi kudanganya!

Ni furaha inayobubujika kutoka katika undani wa mtu, kwa kumkirimia amani na uwezo wa kupenda na kupendwa; Yesu Kristo ni bandari salama, changamoto kwa waamini kumtolea ushuhuda wa furaha na matumaini ya kweli; huruma na msamaha pamoja na kupokea kila hali ya maisha kwa imani na matumaini.

Ni Mwaliko wa kuendeleza majadiliano na ulimwengu na kuwa na mawazo na mwelekeo chanya! Watoto wa Kanisa waoneshe furaha, amani na utulivu sanjari na kuendelea kuwafariji wote wanaoteseka kiroho na kimwili, kwani furaha ya Kristo ndiyo nguvu yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.