2012-12-21 07:37:39

"Msizime kamwe moto wa matumaini licha ya ugumu na ukata wa maisha"


Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milano, Italia, amewaandikia waamini na watu wenye mapenzi mema Jimboni mwake, kutozima kamwe mwanga wa matumaini, licha ya magumu na changamoto nyingi wanazoendelea kukabiliana nazo katika hija ya maisha yao ya kila siku, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo anaendelea kuandamana nao katika safari yao ya maisha. RealAudioMP3

Ni mwaliko na changamoto ya kumkaribisha Kristo katika uhalisia wa maisha yao, wakiwa na imani na matumaini kwamba, kamwe, hawako peke yao! Kwa namna ya pekee, anapenda kuwakumbuka watoto, wazee, wagonjwa na wote ambao wako katika uvuli wa mauti bila kuwasahau wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Kardinali Scola anawaandikia watoto Jimboni mwake, akitaka waandamane naye katika hija ya kumtafuta na hatimaye kumwona Mtoto Yesu anayezaliwa kwa mara nyingine tena katika maisha yao. Noeli, Kanisa linafanya sherehe ya kuzaliwa kwa Mtoto Yesu, Mwana wa Mungu. Hii ndiyo zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu anapenda kumzawadia kila mwanadamu. Zawadi zote ambazo watoto hao watapokea wakati wa sherehe za Noeli ni kielelezo cha ujio wake kati yao!

Kardinali Scola anawakumbuka wagonjwa na wote walioko kufani, katika shida na mahangaiko yao ya ndani, watambue kwamba, kwa hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja nao, kama walivyo wazazi kwa watoto wao. Hii ndiyo Habari Njema ya Wokovu katika kipindi cha Noeli kwa Mwaka 2012.








All the contents on this site are copyrighted ©.