Waziri mkuu Pinda asema, Serikali ya Tanzania inapania kujenga daraja katika Mto Kavuu
ili kuboresha maendeleo
Serikali ya Tanzania imetenga kiasi cha sh. bilioni moja kwa ajili ya kazi za awali
za ujenzi wa daraja la mto Kavuu linalounganisha kata za Mamba, Kasansa, Majimoto,
na kijiji cha Inyonga yalipo makao makuu ya wilaya mpya ya Mlele. Hayo yamesemwa na
Waziri Mkuu Mizengo Pinda Jumatano, Desemba 19, 2012 wakati akizungumza na wakazi
wa kata ya Mamba kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya saba ya ziara yake jimboni
kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
Waziri Mkuu alisema Serikali ina
nia ya kufungua mawasiliano kati ya bonde la Rukwa na mikoa ya kaskazini ambako kuna
uhaba wa chakula. “Bonde hili linasifika kwa uzalishaji mkubwa wa nafaka kwa hiyo
kujengwa kwa daraja hilo ni ukombozi mkubwa wa kufungua soko kwa mazao mnayozalisha
huku,” alisema. Katika mwaka huu wa fedha, barabara ya kutoka Sitalike kupitia Kibaoni,
Majimoto, Mamba hadi Kasansa yenye urefu wa kilomita 33.5 imetengewa sh. milioni 837/-
na kwamba wakandarasi wawili wamekwishapatikana ili kuifanyia ukarabati barabara hiyo.
Kuhusu
barabara ya Majimoto hadi Inyonga yenye urefu wa kilometa 135, Waziri Mkuu alisema
zimetengwa sh. milioni 943/- kwa ajili ya ujenzi wa madaraja katika barabara hiyo.
Alipoulizwa kuhusu kuwepo kwa fedha hizo, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS)
Mkoa wa Katavi, Mhandisi Isaack Kamwelwe alimthibitishia Waziri Mkuu kuwepo kwa fedha
hizo. “Fedha zimeshatengwa na leo nimepokea kibali cha kutangaza zabuni za ujenzi
wa daraja hilo. Zabuni zitatangazwa kuanzia Januari 2013,” alisema.
Kutokuwepo
kwa daraja la Kavuu kunawafanya wakazi waishia bonde la Rukwa (maeneo ya Majimoto
na Mamba) kila wanapotaka kwenda Inyonga, walazimike kupitia Mpanda yaliko makao makuu
ya wilaya yao ambako ni zaidi ya kilometa 350.