Watanzania wanahamasishwa kuchangia katika kujiletea maendeleo yao wenyewe! Serikali
itasaidia kuona juhudi hizi zinazaa matunda yanayokusudiwa!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameahidi kuchangia gharama za ununuzi wa jenereta
kwa ajili ya kata ya Majimoto wilayani Mlele mkoani Katavi ili waweze kuwa na umeme
wa uhakika. Alitoa ahadi hiyo Jumatano, Desemba 19, 2012 wakati akizungumza na wakazi
wa kata ya Majimoto kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya saba ya ziara yake
jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
“Kuna wafanyabiashara wa
hapa Majimoto ambao walikuja kuniona na wakasema wako tayari kuchangia ununuzi wa
jenereta lenye uwezo wa kutoa kilovoti 60 za umeme kwa nyumba kama 300. Wao watoe
milioni 25 wakiwa tayari na mimi nitatoa milioni 25... jaribuni mkae na kupanga namna
ya kuchangia gharama.” “Baada ya muda fulani mtakuta mmemaliza kuchangia, tuwarudishie
wafanyabiashara hela yao ili hilo jenereta liwe la kijiji. Mkilipata, nitawasiliana
na TANESCO ili watupatie nguzo za umeme,” alisema.
Akijibu hoja kuhusu viwanja,
Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa Jimbo la Katavi alisema upimaji wa viwanja ulifanyika
miaka miwili iliyopita na vikapatikana viwanja 270 lakini hadi sasa havijagawiwa kwa
wananchi. Aliwataka viongozi wa kata na wilaya wasimamie zoezi hilo. Hata hivyo, Waziri
Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaonya juu ya ujenzi wa nyumba za makazi na biashara kando
ya barabara kuu. ” Ninawasihi sana mheshimu sheria za barabara... msijenge nyumba
zenu ndani ya hifadhi ya barabara.
Wakati huo huo, Waziri mkuu Mizengo Pinda
ameahidi kutoa mizinga ya nyuki 25 ya kisasa na ya kibiashara kwa ajili ya Kikundi
cha Sanaa cha kata ya Mamba wilayani Mlele mkoani Katavi ili waweze kuzalisha mali
na kujiendesha wenyewe. Alitoa ahadi hiyo Jumatano, Desemba 19, 2012 wakati akizungumza
na wakazi wa kata ya Mamba kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya saba ya ziara
yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
“Nitawapa mizinga
25 ya kuanzia ili muongeze na ile miwili mliyopewa na Dk. Kikwembe (Mbunge wa Viti
Maalum mkoa wa Katavi)... nataka ninyi muwe chachu ya mabadiliko hapa mamba ili vijana
wengine na wazee waige kutoka kwenu,” alisema. Aliwataka wabadili mtazamo wao katika
kufuga nyuki kwa kuweka mizinga ardhini au kwenye mabanda badala ya kuitundika kwenye
miti. “Mnapaswa kufuga kisasa ili muweze kuikagua mara kwa mara, sasa ukiitundika
juu ya mti utaendaje kuchungulia kama nyuki wameingia kwenye mzinga au la? Utajuaje
kama masega yaliyomo yana asali ya kutosha? Alihoji.
Alisema wanapaswa watambue
kwamba nyuki anafugwa kama ilivyo kwa viumbe wengine kama vile kuku, mbuzi, bata au
ng’ombe. “Faida mtakayopata hapa ni kuwa karibu na msitu wa Lyamba lya Mfipa. Tungeweka
mizinga pale chini ya msitu jioni hii, kesho asubuhi mngekuta nyuki wameshaingia
na kuanza kazi,” aliongeza.