Wahudumu wa sekta ya afya ni wajumbe wa furaha na matumaini kwa wagonjwa na maskini
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa
wafanyakazi katika sekta ya afya, Jumatano tarehe 19 Desemba, 2012 ameadhimisha Ibada
ya Misa Takatifu kwa ajili ya wafanyakazi wa sekta ya afya mjini Roma, Ibada iliyofanyika
kwenye Kanisa la Santo Spirito in Sassia.
Katika mahubiri yake amekumbusha
kwamba, Mama Kanisa katika kipindi hiki maalum kuelekea maadhimisho ya Fumbo la Umwilisho,
yaani Siku kuu ya Noeli anaonesha utajiri mkubwa wa Liturujia ya Neno la Mungu unaofumbata
Mpango wa Mungu katika kazi ya Ukombozi.
Mwenyezi Mungu ameonesha huruma na
upendo mkuu, akawaandaa na kuwatuma Manabii kwa nyakati mbali mbali ili kumwandalia
njia Mwanaye Mpendwa. Utukufu wa Mungu umejionesha kwa namna ya pekee kwa maskini
na wanyonge, wale waliokuwa wanabezwa na kudharauliwa na Jamii.
Ili kuweza
kumpokea Mungu anayewatembelea waja wake, kuna haja ya kuwa na imani na matumaini
thabiti kama alivyoonesha Elizabeth; ukosefu wa imani una gharama zake, kama ilivyomtokea
Mzee Zakaria alipotia shaka kuhusu mpango wa Mungu katika maisha na familia yake.
Fundisho kuu linalojitokeza hapa ni kuhusu umuhimu wa Sala hasa wakati huu wa Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani. Waamini wajifunze kusali vyema na kamwe wasijikatie tamaa na kulegea
katika sala. Sala ya Baba Yetu ni muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu na ni sala
ya Kikristo.
Waamini watambue kwamba, Mwenyezi Mungu anawapenda, anawasikiliza
na kuwakirimia katika mahitaji yao hata kama si kama walivyoomba, kwani Yeye ni mwingi
wa huruma na mapendo kwa wote wanaokimbilia kwake. Ulimwengu mamboleo unawahitaji
wajumbe watakaotangaza furaha, amani na matumaini kama alivyofanya Yohane Mbatizaji,
hasa kutokana na ukweli kwamba, kuna watu wamekata tamaa kutokana na athari za myumbo
wa uchumi kimataifa, hawana tena matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.
Askofu
mkuu Zimowski anawaalika wafanyakazi katika sekta ya afya kuwa ni wajumbe na mashahidi
wa huduma ya upendo na mshikamano kwa wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa
Jamii, kama walivyofanya watakatifu Filippo Neri na Mtakatifu Camillo wa Lellis. Ni
watakatifu waliowapokea, wakarimu na kuwatibu wagonjwa, maskini na mahujaji mbali
mbali waliokuwa wanatembelea Roma. Huu ndio wajibu msingi hata kwa wahudumu wa Sekta
ya Afya wanaopaswa kutekeleza huduma hii wakisukumwa na upendo wa Kristo unaowawawajibisha
katika utekelezaji wa majukumu na dhamana ya huduma kwa wagonjwa.
Athari za
myumbo wa uchumi kimataifa zinaanza kuonesha pia makucha yake katika sekta ya afya
kwani Serikali nyingi zinaanza kupunguza bajeti na ruzuku kwa Hospitali kama njia
ya kubana matumizi, lakini zinasahau kwamba, waathirika wakuu ni wagonjwa na familia
zao. Hospitali akama anavyosema Baba Mtakatifu ni Jukwaa la Huduma na Uinjilishaji
Mpya, hapa wagonjwa wanapaswa kukutana na Wasamaria wema wanaowahudumia kiroho na
kimwili.
Kuna haja ya kuwa na huduma makini, sawa na zinazozingatia utu na
heshima ya mwanadamu; maadili, sheria na kanuni za afya. Upendo kwa Mungu na jirani,
kiwe ni kipimo cha huduma kwa wagonjwa na maskini; kwa njia hii wafanyakazi hawa watakuwa
wanasaidia kutekeleza mchakato unaopania kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani,
kwa kutumia hata ile rasilimali kidogo iliyopo kwa ajili ya mafao ya wengi.
Askofu
mkuu Zygmunt Zimowisk anahitimisha mahubiri yake kwa kusema kwamba, maadhimisho ya
Siku kuu ya Noeli yawe ni kikolezo cha kuwamegea jirani furaha na matumaini, kwa kutambua
kwamba, hata wahudumu wa Sekta ya Afya ni wadau wakuu wa dhamana ya Uinjilishaji Mpya,
wanaochangia katika mapambano dhidi ya maradhi duniani.